Habari za Kitaifa

Idara yaonya kuhusu mvua kubwa nchini kwa wiki nzima

Na BENSON MATHEKA April 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAMLAKA ya Hali ya Hewa Kenya (KMSA) imetoa onyo kali kuhusu mvua kubwa inayotarajiwa kunyesha katika maeneo mbalimbali ya nchi kuanzia Aprili 22 hadi Aprili 27, 2026, huku ikionya uwezekano wa mafuriko ya ghafla, upepo mkali na hatari ya radi katika baadhi ya kaunti.

Katika taarifa, KMSA imesema kuwa mvua hiyo inaweza kuongezeka kwa kiwango kikubwa, hasa katika Ukanda wa Pwani, sehemu za Kaskazini Mashariki na Nyanda za Juu za Kusini Mashariki.

Mamlaka hiyo imeeleza kuwa katika baadhi ya maeneo, mvua inaweza kuzidi milimita 20 ndani ya saa 24, hali inayoweza kusababisha mafuriko ya haraka na kuvuruga shughuli za kawaida za wananchi.

Kaunti zilizobashiriwa kuwa katika hatari kubwa ni Kwale, Mombasa, Kilifi, Tana River, Lamu na Garissa, pamoja na sehemu za Wajir, Mandera, Taita-Taveta, Kitui na Makueni.

KMSA imeongeza kuwa maeneo haya yanaweza pia kushuhudia upepo mkali, jambo linaloweza kuathiri usafiri wa baharini na shughuli za uvuvi.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mawimbi ya bahari katika Ukanda wa Pwani yanatarajiwa kupanda hadi zaidi ya mita 2, hali inayoweka hatarini wavuvi na vyombo vidogo vya majini.

Wataalamu wa hali ya hewa wameonya kuwa hali hiyo, inaweza kusababisha hatari kubwa kwa jamii zinazoishi karibu na bahari na mito.

KMSA imewahimiza wakazi wa maeneo husika kuwa katika tahadhari ya juu dhidi ya mafuriko ya ghafla, hasa wale wanaoishi mabondeni na karibu na mito.

Pia, imetahadharisha kuhusu kupungua kwa mwonekano barabarani, jambo linaloweza kuongeza hatari ya ajali za barabarani katika kipindi cha mvua.

Aidha, mamlaka hiyo imeonya kuhusu hatari ya radi, ikiwataka wananchi kuepuka kujikinga chini ya miti au karibu na maeneo ya chuma wakati wa mvua kubwa.

Wananchi pia wameshauriwa kuepuka kuvuka maji yanayosonga kwa miguu au kwa magari, kwani hali hiyo inaweza kuwa hatari na kusababisha vifo.

Kulingana na wataalamu wa hali ya hewa, kipindi hiki ni sehemu ya msimu wa mvua yav masika unaoendelea nchini, ambao mara nyingi huleta changamoto kubwa ikiwemo uharibifu wa miundombinu, kuathirika kwa kilimo na usumbufu wa usafiri.

Katika miaka iliyopita, baadhi ya maeneo yamekuwa yakikumbwa na mafuriko makubwa kutokana na mvua.

Serikali kupitia idara husika imewataka wananchi kufuatilia taarifa rasmi kutoka KMSA na kuchukua tahadhari mapema ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza.

Aidha, serikali za kaunti zimeshauriwa kuimarisha mabomba ya maji mijini na vijijini, pamoja na kujiandaa kwa dharura katika maeneo yanayokumbwa mara kwa mara na mafuriko.

Wakazi wa maeneo ya pwani wametakiwa pia kuwa waangalifu zaidi kutokana na hali ya bahari kuwa hatari, huku wavuvi wakihimizwa kuepuka shughuli za uvuvi wakati mawimbi yatakapokuwa makali.