Serikali yaahidi kuwasaidia waliopoteza mali Gikomba
SERIKALI imewahakikishia wafanyabiashara waliopoteza mali katika kisa cha moto kwenye Soko la Gikomba jijini Nairobi kwamba watapata msaada huku vyombo vya usalama vikianzisha uchunguzi kubaini chanzo cha kisa hicho.
Msemaji wa Serikali Isaac Mwaura alisema serikali inatambua hasara ambayo wafanyabiashara ambao hutegemea soko hilo kwa kujipatia riziki, walipata.
Moto huo uliotokea Jumapili, ulisababisha vifo vya watu wawili, kujeruhi zaidi watu 17 na kuteketeza vibanda vingi vya biashara pamoja na bidhaa za thamani ya mamilioni ya pesa.
Bw Mwaura alieleza kuwa tukio hilo ni pigo kubwa kwa mapato ya wafanyabiashara hao na kuthibitisha kuwa mashirika ya kutoa msaada wa kidharura tayari yamefahamishwa ili yawajibike.
“Serikali inaelewa hasara kubwa wafanyabiashara ambao maisha yao yanategemea biashara za kila siku katika Soko la Gikomba walipata. Tunataka kuwahakikishia kuwa hawataachwa wakabiliane na hali hiyo pekee yao,” alisema Mwaura.
Wakati huo huo, serikali imewataka wananchi kuwa na subira na kuepuka uvumi kuhusu chanzo cha moto huo.
Bw Mwaura alisema uchunguzi wa kina na wa uwazi utafanywa ili kubaini kilichosababisha moto huo, ikiwa ni pamoja na kuchunguza iwapo ulitokana na uzembe au vitendo vya uhalifu.
Aliongeza kuwa matokeo ya uchunguzi huo yatatumika kuimarisha usalama kuhusiana na mikasa ya moto katika masoko mbalimbali nchini na kusaidia kuzuia matukio kama hayo siku zijazo.