Maandamano yachacha kupinga kituo cha Ebola huku watalii nao wakisusia Laikipia
POLISI jana walirusha vitoa machozi na kuwakamata waandamanaji kadhaa waliokuwa wakipinga ujenzi wa kituo cha kutenga wagonjwa wa Ebola kinachofadhiliwa na Amerika katika Kambi ya Jeshi la Angani ya Laikipia, Nanyuki.
Waandamanaji hao walikusanyika karibu na kambi hiyo wakidai kuwa serikali za Kenya na Amerika zinapuuza amri ya mahakama na maoni ya wananchi kwa kuendelea na mradi huo wenye utata mkubwa.
Walioshuhudia walisema polisi walitawanya makundi madogo ya waandamanaji kwa vitoa machozi huku watu sita wakikamatwa na kupelekwa katika magari ya polisi.
Mmoja wa waandamanaji alionekana akiwa amebeba msalaba mweupe ulioandikwa maneno “Respect Ebola” kwa rangi nyekundu.
“Kituo hiki hakifai kujengwa hapa. Kwa nini serikali ijikite katika ugonjwa ambao hatuna ilhali magonjwa yanayotusumbua hayapatiwi suluhu?” alisema Bethwel Onyango, mmoja wa waandamanaji.
Mradi huo wa kituo cha vitanda 50 unalenga kuwaweka karantini raia wa Amerika waliokumbana na virusi vya Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Uganda kwa muda wa hadi siku 21.
Hata hivyo, Wakenya wengi wanahofia kuwa nchi yao inabebeshwa hatari ya kushughulikia ugonjwa huo kwa niaba ya Amerika.
Maandamano hayo yanajiri wiki moja baada ya watu wawili kuuawa katika ghasia zilizotokea Nanyuki kuhusiana na mradi huo.
Wakati huo huo, Kaunti ya Laikipia imewasilisha kesi mahakamani ikidai haikushirikishwa katika maamuzi ya kuchagua eneo la kituo hicho licha ya kuwa na jukumu la afya ya umma na maandalizi ya dharura.
Katika hati iliyowasilishwa mahakamani na Waziri wa Afya wa Kaunti ya Laikipia, Bw Albert Taiti, Kaunti hiyo, ilisema mchakato wa kuanzishwa kwa kituo hicho ulikosa uwazi, mashauriano na ushirikishaji wa umma kama inavyotakiwa na Katiba.
Kaunti hiyo pia imeonya kuwa sekta ya utalii tayari imeanza kuathirika huku hoteli zikianza kupokea kufutwa kwa safari kutoka kwa watalii wanaohofia uwepo wa kituo hicho.
Nanyuki ni kitovu muhimu cha utalii na lango la kuelekea Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kenya pamoja na maeneo kadhaa ya wanyamapori.
Aidha, viongozi wa kaunti wameeleza wasiwasi kuhusu ukaribu wa kituo hicho na shule za Airbase Primary School na Airbase Junior School ambazo ziko ndani ya kambi hiyo ya jeshi.
Mahakama Kuu tayari imetoa amri mara mbili za kusitisha utekelezaji wa mradi huo na kuitaka serikali kufichua makubaliano na taratibu zote za uendeshaji wa kituo hicho.
Hata hivyo, taarifa zinaonyesha kuwa ndege za kijeshi za Amerika zimeendelea kuwasili na vifaa pamoja na wafanyakazi. Kesi hiyo itatajwa tena mahakamani Juni 23, 2026.