Habari za Kitaifa

Mabilioni hatarini kunywa maji miradi mikubwa ikizimwa kwa misingi ya kisheria

Na JOSEPH WANGUI, RUTH MBULA April 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MIRADI kadhaa mikubwa ya serikali imezimwa au kubadilishwa mwelekeo kufuatia maagizo ya mahakama na viongozi wa serikali, hali inayoweka walipa kodi katika hatari ya kupata hasara ya mabilioni na kuibua maswali mapya kuhusu inavyopangwa, ushirikishaji wa umma na uthabiti wa sera.

Matukio ya hivi punde yanahusisha kusimamishwa kwa mradi wa nyumba za gharama nafuu katika Kaunti ya Kiambu na ubomoaji wa miundombinu katika eneo la Gusii, yakionyesha jinsi changamoto za kisheria na mabadiliko ya sera yanavyoathiri mwelekeo wa miradi ya maendeleo ya serikali.

Katika Kaunti ya Kiambu, Mahakama Kuu imesimamisha ujenzi wa mradi wa nyumba nafuu katika eneo la Githunguri, hatua ambayo ni pigo kwa Rais William Ruto katika ajenda yake ya makazi.

Mahakama ilitoa amri kali kusitisha shughuli zote katika kipande cha ardhi cha ekari 58 Kiawairera, eneo lililozua maandamano kutoka kwa wazee wa Kikuyu waliodai ni sehemu yenye historia muhimu ya mapambano ya Mau Mau.

Amri hiyo inakataza serikali au maajenti wake “kuchimba, kuendeleza, kuuza au kuingilia kwa namna yoyote ardhi hiyo” hadi kesi ya kikatiba itakaposikilizwa na kuamuliwa.

Uamuzi huo ulitolewa siku chache baada ya Mahakama ya Ardhi na Mazingira ya Thika kutoa maagizo yanayofanana, hivyo kuimarisha kusitishwa kwa mradi huo.

Mahakama pia iliamuru vifaa vyote, mitambo na ukuta kuondolewa mara moja na ardhi kurejeshwa katika hali yake ya awali, ikisisitiza umuhimu wa kulinda eneo hilo ambalo walalamishi wanasema lina thamani ya kihistoria na kitamaduni.

Walalamishi wanadai kuwa ardhi hiyo ina makaburi ya wapiganiaji uhuru wa Mau Mau, sehemu iliyotumiwa kunyonga wafungwa na maeneo ya zamani ya chuo cha walimu cha Githunguri kilichokuwa kitovu cha mwamko wa kisiasa kabla ya kufungwa mwaka 1952.

Wanasema serikali ilitenga ardhi hiyo kwa mradi wa nyumba bila ushirikishaji wa umma wala kuzingatia sheria za kulinda urithi wa taifa.

Kesi hiyo itatajwa Aprili 28, 2026, na inatarajiwa kuendelea kusikilizwa kikamilifu ili kubaini iwapo mradi huo unaweza kuendelea kisheria.

Wakati huo huo, katika eneo la Gusii, hali imechukua mkondo tofauti ambapo maamuzi ya serikali yamevuruga miradi iliyokuwa ikiendelea.

Katika Kaunti za Kisii na Nyamira, mamilioni ya fedha za umma ziko hatarini kufuatia maagizo ya Rais Ruto kubomoa sehemu za Uwanja wa Gusii na Uwanja wa Ndege wa Suneka.

Uchambuzi unaonyesha kuwa zaidi ya Sh500 milioni zinaweza kupotea kutokana na ubomoaji huo na ujenzi mpya unaotarajiwa.

Katika uwanja wa ndege wa Suneka, Rais aliamuru jengo la abiria lililokamilika kubomolewa akisema halifai.

“Jengo hili linafanana na nyumba ya makazi. Nimeamuru libomolewe na kujengwa jipya,” alisema.

Aidha, aliagiza uwanja huo ujengwe upya na barabara ya ndege iongezwe kutoka mita 900 hadi zaidi ya kilomita moja.

Alimtaka Waziri wa Uchukuzi Davis Chirchir kusimamia ujenzi wa jengo jipya na upanuzi huo ndani ya miezi
Uwanja wa Suneka ulikuwa umeboreshwa awali kwa Sh52 milioni, huku mpango mwingine wa Sh132 milioni ukipangwa kabla ya uchaguzi wa 2022.

Hata hivyo, mradi huo umekuwa ukibadilishwa mara kwa mara, kwani hapo awali Rais alikuwa ameusimamisha na kupendekeza ujenzi wa nyumba nafuu badala yake.

Katika uwanja wa Gusii, Rais aliamuru ubomoaji na ujenzi mpya wa uwanja wa kisasa wenye uwezo wa kubeba watu 14,000 kwa gharama ya Sh1 bilioni.

Uwanja huo, uliokuwa umejengwa wakati wa gavana wa zamani James Ongwae, tayari ulikuwa umegharimu pesa nyingi katika ukarabati wa mara kwa mara.

Mwaka 2024 pekee, takriban Sh34 milioni zilitumika kuuboresha, huku serikali ya kitaifa na kaunti zikiwekeza zaidi ya Sh200 milioni katika miaka iliyopita.

Licha ya uwekezaji huo, uwanja huo umefungwa mara kadhaa tangu 2014 kutokana na ukarabati usioisha.

Miradi hiyo pia imekuwa ikitumika kwa hafla za kitaifa kama Maadhimisho ya Mashujaa Dei na michezo ya kitaifa, lakini mabadiliko ya mara kwa mara yameibua wasiwasi kuhusu mipango ya muda mrefu.