Vinywaji vyenye sukari ya juu huchangia upara kwa wanaume – Watafiti
KUNYWA zaidi ya kinywaji kimoja chenye kiwango cha juu cha sukari kila siku kunaongeza hatari ya kupoteza nywele na kuwa na upara miongoni mwa wanaume, watafiti wamebaini.
Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Tsingua, Beijing, China unaonyesha kuwa viwango vya juu vya sukari vina athari ya moja kwa moja katika kupandisha kiwango cha homoni na kutanua mishipa mwilini.
Homoni kupanda huathiri afya ya nywele na kutatiza kumea kwake pamoja na kukatika kwa zile ambazo zimemea.
Kunywa vinywaji vyenye sukari nyingi husababisha mwili kukataa kiwango cha juu cha insulini.
Hali hii pia huchangia kongosho kutoa insulini kwa kiwango cha juu zaidi ili kudhibiti sukari kwenye damu na ikilemewa, huchangia mtu kupata ugonjwa wa sukari.
Kando na maradhi hayo ya sukari, kiwango cha juu cha insulini pia huhusishwa na kuathiri jinsi nywele zinavyomea.
Pia vinywaji au vyakula vyenye sukari nyingi huhusishwa na mwili kukosa usawazishaji wa madini na hufanya nywele kuwa dhaifu zinapomea na kuchuchuka.
“Kunywa vinywaji vyenye sukari nyingi huandamana na pia mlo ambao mara nyingi una mafuta. Utafiti umeonyesha kuwa kiwango cha juu cha mafuta kinachangia kupotea kwa nywele,” akasema Dkt Ken L. WilUtafiutliam Jr ambaye alishiriki katika utafiti huo.
“Hata madaktari wa upasuaji wanaopandikiza nywele wanaelewa kuwa mtindo wa ulaji huchangia afya ya mgonjwa. Kufanya mazoezi, kuepuka mihadarati na dawa nyingine za kulevya zinachangia mgonjwa kuishi kwa kipindi kirefu,” akaongeza.
Hata hivyo, utafiti huu unahitaji kuzama zaidi kwa sababu pia imebainishwa kuwa msongo wa mawazo, mtindo wa maisha kijumla na jeni pia huchangia nywele kupotea.
Kula vyakula vyenye madini muhimu na kushiriki mazoezi hutekeleza wajibu muhimu katika kusaidia nywele kumea.