Maswali Ruto akidandia mradi uliozinduliwa na Nyoro
Maswali yanaibuka kuhusu kile ambacho wakosoaji wanataja kuwa juhudi za Rais William Ruto kujipigia debe kwa miradi iliyoanzishwa na viongozi wengine, kufuatia ziara yake ya siku mbili katika Kaunti ya Murang’a.
Kiini cha mzozo huo ni Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Kiufundi cha Kiharu (TVET), ambacho kimezua mvutano mkali wa kisiasa kuhusu uzinduzi na umiliki wake. Wakati wa ziara yake Ijumaa, Rais Ruto alizindua kituo cha ICT na pia kuanzisha ujenzi wa mabweni ya wanafunzi, akieleza kuwa ni sehemu ya uwekezaji wa serikali katika elimu ya kiufundi.
Hata hivyo, kuna maswali kuhusu msururu wa matukio. Mnamo Machi, Ndindi Nyoro alizindua rasmi taasisi hiyo baada ya kukamilika kwa jengo la masomo la Mwai Kibaki, hatua iliyoweka msingi wa kuanza kwa shughuli za chuo hicho wiki kadhaa kabla ya ziara ya Rais.
Hali hii imezua mjadala iwapo Rais alianzisha hatua mpya ya maendeleo au aliwasilisha upya mradi uliokuwa tayari umeanzishwa. Mjadala huo ulizidi kushika kasi baada ya video kuibuka zikionyesha kuwa kibao kilichoonyesha uzinduzi wa awali wa Nyoro kilifunikwa wakati wa ziara ya Rais.
Kutokuwepo kwa Nyoro katika hafla hiyo pia kumeongeza gumzo, hasa ikizingatiwa kuwa hapo awali alikuwa mshirika wa karibu wa Rais. Aliwahi kuwa mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti na Matumizi ya Bunge kabla ya kuanza kukosoa baadhi ya sera za serikali.
Mvutano huo ulidhihirika zaidi wakati Waziri wa Ardhi, Bi Alice Wahome alipomshauri Nyoro arejee serikalini, kauli iliyokumbana na upinzani kutoka kwa baadhi ya wananchi.
Akijibu wakosoaji, Rais Ruto alikashifu wapinzani wake akisema: “Wale jamaa wanajaribu kushindana na sisi ni watu wa matusi mengi, kisirani mingi, hasira mingi, lakini kazi hawajui, mpango hawana, ajenda hawana, sera hawana. Ni kweli ama si kweli?” Pia alisisitiza dhamira yake ya maendeleo akisema: “Ata waniite Kasongo, si barabara inaendelea, pamoja na shule na stima? Niendelee ama nisiendelee?”
Kwa upande wake, Naibu Rais Kithure Kindiki aliwahimiza wafuasi kumuunga mkono Rais kwa akisema: “Ni tutam si tutam? Rais Ruto aendelee asiendelee?”
Naye Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa, Kimani Ichung’wah, alipuuzilia mbali ukosoaji akisema: “Najua matusi umetukanwa vile sisi tumetukanwa. Lakini hata tukiitwa watoto tutazingatia maisha ya wananchi wa Kenya.”
Baada ya ziara ya Rais, baadhi ya wakazi walionekana wakiharibu vifaa vyenye nembo ya UDA, ishara ya mabadiliko ya hisia za kisiasa katika eneo la Mlima Kenya.
Viongozi wa upinzani, akiwemo Rigathi Gachagua, wamekosoa serikali wakidai kuwa ziara hizo zinatumika kwa propaganda za kisiasa na uzinduzi wa miradi isiyokuwa na bajeti.
Licha ya mzozo huo, Rais Ruto alizindua miradi mingine kadhaa Murang’a, ikiwemo nyumba za bei nafuu huko Kandara na Gatanga pamoja na barabara Mathioya ili kuboresha usafiri na biashara.
Alikamilisha ziara hiyo kwa kukagua masoko na kusaidia wakulima wa maziwa, akisisitiza kuwa maendeleo yataendelea licha ya ukosoaji.