Ubaguzi wa rangi bado umekithiri Zambia miaka 60 baada ya uhuru
BAADHI ya raia wa Zambia wanakumbwa na tatizo la ubaguzi wa rangi, zaidi ya miaka 60 baada ya kupata uhuru kutoka Uingereza.
Zambia hujivunia kuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya ukoloni.
Hata hivyo, mara nyingi ubaguzi wa rangi hujitokeza waziwazi, na huwafanya wajihisi kama raia wa daraja la pili katika nchi yao wenyewe.
Kutokana na simulizi zao, matukio hayo hujitokeza kwenye nafasi za kazi ambapo Waafrika wamepuuzwa.
Tatizo lingine ni kutohudumiwa ipasavyo katika mikahawa, na hata kudhalilishwa na baadhi ya wamiliki wa nyumba.
Hata hivyo, pia kuna matumaini, huku baadhi ya Wazambia wakifurahishwa na ukweli kwamba mazungumzo kuhusu masuala ya rangi yanaanza kufanyika kwa uwazi zaidi.
Serikali ya Zambia, kwa upande wake, ilikanusha kuwa ubaguzi wa rangi ni tatizo nchini humo.
Alexander Bwalya ambaye ni raia mweusi wa Zambia alisema ni jambo la ajabu sana kwamba watu wanaweza kuishi katika nchi ya Afrika na bado wawe na ubaguzi dhidi ya watu weusi.
“Kuna wazungu waliofika hotelini na wakaanza kuhudumiwa mbele yetu na tulipolalamika kwa meneja, tuliambiwa, kama hatujaridhika na huduma, tuko huru kuondoka.”
Haya yanajiri zaidi ya miongo sita tangu Kenneth Kaunda, mmoja wa viongozi waliopambana dhidi ya ukoloni barani Afrika, alipokuwa rais wa kwanza wa Zambia.
Kabla ya uhuru mwaka 1964, Wazambia weusi walilazimika kubeba vibali vilivyodhibiti mienendo yao. Shule na hospitali zilikuwa zimetengwa kwa misingi ya rangi, na kazi za kitaalamu zenye mishahara mikubwa katika migodi ya shaba zilihifadhiwa kwa wafanyakazi weupe pekee.