Habari za Kitaifa

Murkomen, Sudi na Kururia wahusishwa na unyakuzi wa ardhi Runda

Na SIMON CIURI April 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAZIRI wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen, Mbunge wa Kapseret Oscar Sudi na mwenzake wa Gatundu Kaskazini Elijah Kururia wamehusishwa katika mzozo mkali wa muda mrefu wa kifamilia kuhusu ardhi ya kifahari katika eneo la Runda, inayojumuisha kituo maarufu cha burudani cha Paradise Lost.

Daniel Mwangi Mbugua na binti yake Wanjiru Mwangi wameomba Mahakama Kuu ya Kiambu iamuru Tume ya Maadili na Kukabili Ufisadi (EACC) kuwachunguza viongozi hao watatu kwa madai ya kuhusika katika unyakuzi wa ekari 300 za ardhi yenye thamani inayokadiriwa kufikia Sh20 bilioni.

Ardhi hiyo, iliyosajiliwa kama LR 5974/1, 5972 na 5971, ni sehemu ya mali iliyoachwa na mfanyabiashara tajiri wa Kiambu marehemu Mbugua Mwangi, aliyekuwa akimiliki mali nyingi kupitia kampuni ya Ndunde Investments.

Marehemu huyo, aliyefariki mwaka wa 2008, pia alimiliki mashamba ya kahawa ya Misahara na Kasarini pamoja na mali nyingine katika maeneo ya Kangemi, Runda, Ruiru na Karen.

Katika hati zilizowasilishwa mahakamani, Bw Mbugua na binti yake wanadai kuwa viongozi hao wanawalinda zaidi ya watu 200 wanaodaiwa kuvamia ardhi hiyo na kuanza kuimiliki kinyume cha sheria.

Pia, wanadai kuwa sehemu ya ardhi hiyo imehamishiwa kampuni ya Pamat Enterprises Limited.

Walalamishi wameeleza kuwa baadhi ya maafisa wa polisi katika kituo cha Kiambu wameshawishiwa, wakidai kuwa wamekuwa wakishirikiana na watu wanaodaiwa kuvamia ardhi hiyo.

Wanasema pia kuwa kumekuwa na mikutano ya kupanga njama za kuwanyima urithi wao wa kifamilia.

Aidha, Bw Mbugua amewataja ndugu zake wawili, Isaac Gichia Mbugua na Joseph Mbai Mbugua, kama wahusika wenye maslahi katika kesi hiyo, akiwalaumu kwa kushirikiana na wanaodaiwa kunyakua ardhi ili kumtenga yeye na binti yake katika urithi huo.

Hata hivyo, ndugu hao wamekanusha madai hayo, wakisema wao pia ni waathiriwa wa unyakuzi wa ardhi hiyo.

Kwa upande wake, Mbunge Elijah Kururia alikanusha madai hayo akisema kuwa baadhi ya wakazi walipewa ardhi hiyo na serikali katika miaka ya 1980, huku kampuni ya Pamat Enterprises Limited pia ikipewa sehemu yake kihalali.

Aliongeza kuwa hakuna uvamizi wa Paradise Lost kama inavyodaiwa, na kwamba walalamishi hawafahamu mipaka halisi ya ardhi wanayodai.

Mahakama Kuu ya Kiambu imewaagiza walalamishi kuwapa wahusika wote stakabadhi za kesi kabla ya tarehe ya kutajwa kwa kesi hiyo Mei 19, 2026, ambapo mwongozo zaidi utatolewa.

Katika madai yao, Bw Mbugua na binti yake pia wamedai kuwa maisha yao yako hatarini, wakisema kulikuwa na vitisho na hata jaribio la kuwashambulia Aprili 13, 2026.

Bi Wanjiru alidai kuwa alimuona Waziri Murkomen katika eneo hilo akiwa na msafara wa magari na watu wenye silaha.

Kesi hiyo inaangazia pia changamoto pana ya unyakuzi wa ardhi nchini, ambapo watu binafsi na kampuni zimekuwa zikidai umiliki wa mali kupitia nyaraka tata, hali ambayo imezua kesi nyingi mahakamani.

Rekodi za Huduma ya Usajili wa Biashara zinaonyesha kuwa kampuni ya Pamat Enterprises Limited ilisajiliwa mwaka wa 1984 na inaendesha shughuli zake kutoka eneo la Lavington, Kaunti ya Nairobi.

Wakurugenzi na wenyehisa wake ni Philip Mulwa Nzioka, Isaya Begi Gesicho, Black Scorpion International Services Limited, ICPHER Consultants Co Ltd na Dawn Innovations.

Afisa mmoja wa kampuni hiyo aliahidi kujibu maswali yaliyoelekezwa kwao, lakini kufikia wakati wa kuchapishwa kwa taarifa hii, hakukuwa na majibu yoyote.

Unyakuzi wa ardhi nchini Kenya umeongezeka kwa kiwango kikubwa, huku baadhi ya watu wakijifanya wamiliki halali wa mali kupitia nyaraka tata.

Hali hii imesababisha kufunguliwa kwa kesi nyingi mahakamani pamoja na uchunguzi wa kina kuhusu udanganyifu, hasa katika sekta ya ununuzi wa nyumba kabla ya kukamilika.

Katika baadhi ya matukio, wanunuzi hugundua kuwa wamedanganywa baada ya kufanya uchunguzi wa kina kuhusu ardhi au wauzaji, mara nyingi baada ya miradi ya ujenzi kusimama ghafla.

Hali hiyo imewalazimu wanunuzi wengi kushtaki kampuni za uuzaji wa nyumba kwa madai ya udanganyifu na upotoshaji.