Habari za Kitaifa

Mwanahabari mzoefu Macharia Gaitho atekwa nyara akiwa katika kituo cha polisi Karen

Na BENSON MATHEKA July 17th, 2024 Kusoma ni dakika: 1

MWANAHABARI wa miaka mingi  wa masuala ya  kisiasa Macharia Gaitho ametekwa nyara na watu wanaoaminiwa kuwa maafisa wa usalama akiwa katika kituo cha polisi cha Karen, Nairobi.

Inasemekana mwanahabari huyo mzoefu alikuwa na mwanawe katika gari lake walipozuiwa na gari aina ya Subaru wakiondoka nyumbani.

Aliendesha gari hadi kituo cha polisi cha Karen ambapo alitolewa kwa nguvu kutoka gari lake na watu waliovalia kiraia ambao walimsukuma kwa nguvu ndani ya gari jingine na kuondoka naye hadi eneo lisilojulikana.

Katika video iliyosemekana kunaswa na mwanawe, watu wapatao watano wanaonekana wakimsukuma mwanahabari huyo ndani ya gari linalofanana na Probox ndani ya kituo cha polisi huku maafisa katika kituo hicho wakimtazama tu.