Habari za Kitaifa

ODM machozi tu, yadai kupigwa kumbo na UDA katika fidia ya waathiriwa wa maandamano

Na MOSES NYAMORI June 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MVUTANO wa wazi kati ya chama tawala cha UDA na ODM kuhusu fidia kwa waathiriwa wa maandamano ulijitokeza katika Ikulu Jumatatu iliyopita baada ya Seneta Oburu Oginga kulalamikia kile alichodai ni kutengwa kwa chama chake.

Dkt Oginga, ambaye ni kinara wa ODM, alimwambia hadharani Rais William Ruto kuwa mwaliko wake kuhudhuria hafla ya kupokelewa kwa ripoti ya Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu (KNCHR) kuhusu mfumo wa kufidia waathiriwa wa ukiukaji wa haki za binadamu ulionekana kutolewa dakika za mwisho.

Imebainika kuwa Dkt Oginga alipokea mwaliko wa kuhudhuria hafla hiyo Jumatatu asubuhi na alipowasili shughuli zilikuwa tayari zimeanza. Viongozi kutoka mihimili yote mitatu ya serikali – Serikali Kuu, Bunge na Mahakama – walikuwa wamehudhuria.

Mbali na Dkt Oginga, Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohammed ndiye afisa mwingine pekee wa ODM aliyekuwa Ikulu.

Baadhi ya maafisa wa ODM walidai Bw Mohammed alihudhuria kwa bahati tu baada ya kufika Ikulu kushuhudia kutiwa saini kwa Mswada wa Ugavi wa Mapato wa 2026, huku maafisa wa Ikulu wakisema alialikwa kama sehemu ya uongozi wa Bunge.

Fidia kwa waathiriwa wa maandamano ilikuwa mojawapo ya ajenda 10 zilizotiwa saini kati ya Rais Ruto na aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga Machi 7, 2025.

Viongozi wa ODM wanaamini chama hicho kinapaswa kushirikishwa kikamilifu katika utekelezaji wa mpango huo kama ishara ya nia njema.

Makubaliano ya kisiasa kati ya UDA na ODM yanategemea ajenda hiyo ya vipengele 10 inayolenga kuongoza mageuzi katika utawala, ushirikishaji wa kiuchumi, uaminifu uchaguzini na uwajibikaji wa taasisi za umma.

ODM imekuwa ikitumia ahadi ya kufidia familia za waliouawa na waliojeruhiwa na polisi wakati wa maandamano ya kupinga serikali kuvutia wafuasi wake kuunga mkono serikali jumuishi na hata uwezekano wa kumuunga mkono Rais Ruto katika uchaguzi mkuu ujao.

Alipopewa nafasi ya kuzungumza, Dkt Oginga hakusita kueleza kutoridhishwa kwake na jinsi ODM ilivyoshughulikiwa katika hafla hiyo.

“Kwanza kabisa, Mheshimiwa Rais, ningependa kusema sikuandaliwa ipasavyo kwa hafla hii. Sijui kwa nini sikualikwa kwa wakati unaofaa, lakini sitaki kulalamika,” alisema.

Aliendelea kusema kuwa huenda hali hiyo ilitokana na kutokuwapo kwa ndugu yake Raila Odinga.

“Nadhani ni kwa sababu ndugu yangu hayupo. Angekuwepo nina hakika angekuwa wa kwanza kualikwa kwa sababu alithamini sana masuala ya haki za binadamu,” alisema.

Baadaye Dkt Oginga alieleza kuwa mpango wa kufidia waathiriwa ni mradi uliokuwa karibu sana na moyo wa Bw Odinga.

“Kwa ushirikiano na serikali nitahakikisha kila mtu anayestahili anafidiwa. Kwa familia zilizopoteza wapendwa wao, tafadhalini pokeeni hili kama ishara ya majuto; ingawa maisha ya binadamu hayawezi kulipwa kwa fedha, ni hatua muhimu kuelekea haki,” alisema.

Bw Mohammed alikataa kutoa maoni kuhusu suala hilo alipofikiwa na wanahabari wetu.

Hata hivyo, afisa mmoja wa ODM alisema Bw Mohammed na mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Bunge walifahamishwa kuhusu mkutano huo walipofika Ikulu kwa shughuli ya kutiwa saini kwa Mswada wa Ugavi wa Mapato.

“Hakuna afisa wa chama aliyealikwa. Manaibu viongozi wa chama, Magavana Simba Arati wa Kisii na Abdulswamad Nassir wa Mombasa pamoja na mwenyekiti wa chama Gladys Wanga hawakupata mwaliko,” alisema afisa huyo.

Jinsi hafla hiyo ilivyoandaliwa imezua mjadala mkali ndani ya ODM, huku baadhi ya viongozi wakidai kuwa kuna njama ya UDA na Rais Ruto kujijenga na mpango wa fidia.

Suala hilo lilijadiliwa katika kikao cha Kamati Kuu ya Usimamizi ya ODM kilichofanyika Jumatatu jioni na kuhudhuriwa na Dkt Oginga, Magavana Arati, Wanga na Nassir, Bw Mohammed, Naibu Katibu Mkuu Catherine Omanyo, Gavana wa Wajir Ahmed Abdullahi na Mweka Hazina Timothy Bosire miongoni mwa wengine.

“Fidia hii ilikuwa wazo la ODM na inamilikiwa kwa pamoja na vyama vyote viwili,” alisema mmoja wa waliohudhuria kikao hicho.

Aliongeza kuwa kauli ya Rais Ruto kwamba rafiki yake alimuonya kuwa kufidia waathiriwa kungeonekana kama kukiri makosa ilionyesha juhudi za kuufanya mpango huo kama ni wa kibinafsi.

“Hotuba ya Oburu ilikuwa ishara tosha kuwa chama hakijafurahishwa na jinsi suala hili linavyoshughulikiwa,” alisema.

Kwa upande mwingine, afisa mmoja wa Ikulu aliyezungumza kwa sharti ya kutotajwa jina alisema mpango wa awali ulikuwa KNCHR iwasilishe ripoti yake kwa Rais katika kikao kidogo cha ofisini Ijumaa, lakini Rais akaagiza hafla ya hadhara kufanyika Jumatatu.

Alisema mkanganyiko ulitokea baada ya mwaliko kutolewa kwa viongozi wa Bunge na Mahakama pekee, akifichua pia kuwa Rais mwenyewe alimpigia simu Dkt Oginga Jumatatu asubuhi kuuliza kama alikuwa amealikwa.

“Lengo lilikuwa kikao kidogo cha kuwasilisha ripoti, lakini Rais alisema kwa kuwa suala hilo linahusu fedha za umma lifanywe hadharani,” alisema afisa huyo.

Katika hotuba yake, Rais Ruto alisema mpango huo unatokana na imani ya pamoja kwamba Kenya haiwezi kuendelea kupitia maumivu yale yale kizazi baada ya kizazi na maandamano baada ya maandamano.

Ripoti hiyo inahusu ukiukaji wa haki za binadamu uliotokana na maandamano miaka ya 2017, 2022, 2023, 2024 na 2025, yakiwemo maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha na yale ya vijana wa Gen Z pamoja na maandamano ya Saba Saba.