Habari za Kitaifa

Quickmart yakanusha maafa yalitokea maduka yake OTC, Ruiru

Na CECIL ODONGO June 26th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

USIMAMIZI wa Duka la Jumla la Quickmart umekanusha kuwa maafa yalitokea baada ya matawi yake mawili kuvamiwa na waandamanaji mnamo Jumatano katika kaunti za Nairobi na Kiambu.

Kupitia taarifa, usimamizi wa duka hilo ulikiri kuwa matawi yake ya OTC katikati mwa jiji la Nairobi na Ruiru, Kaunti ya Kiambu, yalivamiwa na waandamanaji ambao walishiriki uporaji na uharibifu wa mali.

Hata hivyo, ulikanusha ripoti zilizozagaa mitandaoni kuwa kuna watu waliofariki au kujeruhiwa ndani ya maduka hayo mawili kwenye patashika za uporaji.

“Kinyume na ripoti zinazoenea mitandaoni, tunahakikishia umma kuwa hakuna mfanyakazi wetu, mteja au mtu yeyote ambaye alijeruhiwa au kufa kwenye maduka hayo mawili,” ikasema taarifa hiyo.

Uongozi wa Quickmart ulikiri kuwa maandamano ya Jumanne yalivuruga shughuli zao za kibiashara lakini ukasisitiza kuwa unafanya juu chini kuhakikisha huduma zinarejelewa kama kawaida.

“Tunashiriki katika mikakati yote kuhakikisha huduma zinaendelea kwa wateja wetu na pia wafanyakazi,” ikaongeza.

Wateja wa maduka hayo mawili yaliyoathirika walishauriwa kununua bidhaa kwenye matawi mengine Quickmart karibu nao, kabla ya huduma kurejelewa kama kawaida.

Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen akihutubu Alhamisi, alifichua kuwa Wakenya 10 walipoteza maisha yao wakati wa maandamano hayo yaliyotikisa nchi.

Bw Murkomen aliongeza kuwa zaidi ya watu 400 walijeruhiwa, 300 kwenye idadi hiyo wakiwa maafisa wa usalama.

Mashirika ya Kijamii, Shirika la Kimataifa la Amnesty liliweka idadi hiyo kuwa watu 16 na zaidi ya majeruhi 500.