Habari za Kitaifa

Ruto alivyokutana na janga linaloendelea la uhuni katika mkutano wake Emurua Dikirr

Na VITALIS KIMUTAI August 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

GHASIA za kisiasa zilitia doa ziara ya Rais William Ruto katika Kaunti ya Narok Jumatano, baada ya watu wasiopungua sita kujeruhiwa kwa mishale huku wengine kadhaa wakipata majeraha katika mapigano kati ya wafuasi wa Mbunge wa Emurua Dikirr, David Keter na mpinzani wake wa kisiasa Bernard Ng’eno.

Fujo hizo zilitokea katika kituo cha biashara cha Mamboleo kabla ya hafla ya rais kuanza, hali iliyomlazimu Dkt Ruto kuwakemea viongozi hao hadharani na kuwataka kumaliza tofauti zao za kisiasa mara moja.

Wafuasi wa pande hizo mbili walikabiliana kwa kutumia silaha kali ikiwemo mishale.

Afisa mmoja wa polisi kutoka Narok, aliyeomba kutotajwa jina alithibitisha tukio hilo na kusema vurugu vilisababishwa mapigano kati ya vikundi vya wafuasi wa viongozi hao wawili kabla ya Rais kuwasili.

Kwa mujibu wa afisa huyo, waliojeruhiwa walipelekwa katika Hospitali ya St Clare’s Kaplong katika Kaunti jirani ya Bomet, huku mmoja akihamishiwa Hospitali ya South Rift mjini Kericho kwa matibabu maalumu.

Mmoja alikuwa na mshale uliopenya karibu na taya na alitarajiwa kufanyiwa upasuaji.

Wengine walijeruhiwa miguuni, mkononi, begani na mmoja alinusurika kupoteza jicho baada ya mshale kupenya karibu na paji la uso.

Vurugu hizo zilimfanya Rais Ruto kutoa onyo kali dhidi ya siasa za uhasama. Katika mikutano yake mbalimbali, aliwataka viongozi kuacha tofauti zao na kuzingatia maendeleo ya wananchi.

“Aina ya tofauti za kisiasa zinazochochea vurugu, majeraha na umwagaji damu hazipaswi kuruhusiwa. Ghasia hizi lazima zikome mara moja,” alisema Rais.

Aliwataka viongozi kutambua kuwa uchaguzi unapokwisha, wajibu wao ni kuwaunganisha wananchi badala ya kuwagawanya.

Rais pia alimhimiza Mbunge Keter kuchukua jukumu la kuwaleta pamoja wakazi wa Emurua Dikirr na kuzima migawanyiko iliyojitokeza wakati wa uchaguzi mdogo wa Mei mwaka huu.

Wafuasi wa Ng’eno walionekana wakipeperusha vitambaa vya rangi ya samawati wakati wa mikutano ya rais huku wale wa Keter wakionyesha rangi za chama cha UDA, jambo lililoonyesha wazi mgawanyiko uliopo katika eneo hilo.

Dkt Ruto pia alimpongeza Ng’eno kwa kubaki ndani ya chama cha UDA licha ya kushindwa katika kura za mchujo na kumhimiza kuendelea kushirikiana na viongozi wengine kwa manufaa ya wananchi.

Katika kura za mchujo za UDA zilizofanyika Machi 27, Keter alipata kura 13,749 dhidi ya kura 13,394 za Ng’eno.

Baadaye katika uchaguzi mdogo wa Mei 14, Keter alishinda kiti hicho kwa kura 18, 266.

Tukio hilo limeibua upya wasiwasi kuhusu ongezeko la makundi ya wahuni wa kisiasa huku taifa likielekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.