Siasa

Vinara wa Upinzani wakosa kutoa majibu kuhusu atakayebeba bendera 2027

Na JUSTUS OCHIENG August 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KIKAO cha vinara wa upinzani kilichotarajiwa kutoa mwelekeo mpya wa kisiasa kuelekea uchaguzi wa 2027 kilimalizika Kiambu Jumatatu bila kutatua baadhi ya masuala muhimu yanayotishia juhudi za kuunda muungano mmoja wa kisiasa.

Kikao hicho kilichopangwa kufanyika kwa siku mbili, Agosti 24 na 25, kilimalizika baada ya siku moja.

Muungano huo unahusishwa na kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, naibu kiongozi wa Jubilee Fred Matiang’i, kiongozi wa PLP Martha Karua, kiongozi wa Democratic Party Justin Muturi, Eugene Wamalwa wa DAP-Kenya na Peter Munya wa PNU.

Viongozi hao walitia saini ahadi ya umoja na kukubaliana kumuunga mkono atakayeteuliwa kuwa mgombea wao wa urais.

Hata hivyo, maswali muhimu kuhusu muungano huo bado hayajajibiwa.

Yanahusu nani atakayeongoza muungano, afisi ya usimamizi itaundwaje, maamuzi yatafanywa kwa njia gani na mgombea wa urais atachaguliwa vipi.

Hakukuwa na mwafaka kuhusu kubadilisha jina la Azimio wala jina jipya la muungano, ingawa Komboa Kenya Coalition bado inaonekana kuwa chaguo linalopendelewa na baadhi ya viongozi wa upinzani.

“Kenya kwanza. Umoja badala ya mgawanyiko. Huduma badala ya madaraka,” viongozi hao walisema katika taarifa yao.

Lakini kando na picha hiyo ya umoja, tofauti za kisiasa zinaendelea kujitokeza.

Bw Gachagua hakuhudhuria kikao hicho na badala yake alimtuma naibu wake Cleophas Malala kumwakilisha.

Duru zilisema Bw Gachagua alikerwa na matamshi ya Rais mstaafu Uhuru Kenyatta katika kumbukumbu za aliyekuwa Makamu wa Rais Michael Wamalwa, ambapo alimtaja Bw Musyoka, Dkt Matiang’i na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kama baadhi ya wanasiasa wanaoweza kumkabili Rais William Ruto.

Bw Gachagua, kwa mujibu wa duru hizo, hakufurahishwa na kutotajwa licha ya jukumu lake kubwa katika muungano huo.

Pia kulikuwa na sintofahamu kuhusu kuhudhuria kwa Bw Musyoka. Baadhi ya watu wa karibu naye walidai alifika katika kikao hicho dakika za mwisho.

Muungano huo pia bado hauna afisi inayofanya kazi kikamilifu.

Duru za upinzani zilisema hakuna makubaliano kuhusu namna ya kumpata mgombea wa urais kwa sababu viongozi hao bado hawajajadili ripoti ya kiufundi iliyowasilishwa mapema mwaka huu.

Hilo ni suala nyeti kwa kuwa karibu viongozi wote wakuu wa muungano huo wana matamanio ya urais au wana wafuasi wanaoamini kuwa wanafaa kumkabili Rais Ruto.

Bw Gachagua alisema uteuzi wa mgombeaji urais unapaswa kufanyika baadaye.

“Tutazungumzia mgombeaji wetu baada ya Krismasi. Hauwezi kusukuma mgombeaji atajwe sasa ilhali hauna idadi kubwa( ya wafuasi) na haujaanza kuhamasisha watu,” alisema.

Bi Karua, Bw Wamalwa na Dk Matiang’i pia wanaendelea kuwa na ushawishi katika siasa za upinzani, huku umaarufu wa Bw Sifuna ukiongeza sura mpya katika mjadala wa urithi wa kisiasa.

Hata hivyo, viongozi hao wanasisitiza kuwa swali la mgombea wa urais linaweza kusubiri.

“Kuchagua mgombea mmoja wa urais ndilo jambo rahisi zaidi kati ya changamoto zote tulizo nazo. Tunaweza kukutana siku moja kwa chakula cha mchana na kabla ya chakula cha jioni tukawa tayari tuna mgombeaji,” alisema Bw Gachagua.

Lakini changamoto za muungano hazikomei kwa uteuzi wa mgombea.

Viongozi wanapaswa kukubaliana kuhusu nani atafanya maamuzi, iwapo maamuzi yatafanywa kwa makubaliano au kura, nani atasimamia afisi ya usimamizi na namna mizozo itakavyotatuliwa.

Muungano huo pia unakabiliwa na ushindani wa kisiasa katika Mlima Kenya, ambako DCP ya Bw Gachagua inajaribu kujijenga kama chombo kikuu cha kisiasa.

Kuanzishwa kwa People’s Party of Kenya na Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro baada ya kuondoka UDA ya Rais Ruto kumeongeza ushindani kuhusu chama kitakachodhibiti kura za eneo hilo.

Kwa sasa, kikao cha Windsor kimezalisha tamko la umoja, lakini bado hakijaunda mfumo wa kisiasa unaoweza kudumishwa.
Jaribio kubwa litakuwa wakati viongozi hao wataanza kugawana madaraka.

Nani atakuwa sura ya muungano? Nani atadhibiti shughuli zake? Ni chama kipi kitapata nafasi gani? Na nini kitatokea viongozi wakuu wakitofautiana?

Muhimu zaidi, ni yupi kati ya viongozi hao atakubali kumwachia mwingine azma ya kumkabili Rais Ruto mwaka 2027?