Linda Mwananchi inaponyoka Sifuna? Msajili asema ‘Linda’ na ‘Mwananchi’ yashachukuliwa
MSAJILI wa Vyama vya Kisiasa, John Cox Lorionokou, amefichua kuwa vyama viwili vinavyobeba maneno muhimu yanayotumiwa na vuguvugu la Linda Mwananchi Movement tayari vimo katika mchakato wa usajili wa vyama vya kisiasa.
Ufichuzi huo unaweza kutatiza juhudi za Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na washirika wake za kubadilisha vuguvugu hilo kuwa chama cha kisiasa kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.
Moja ya vyama hivyo ni Liberty National Democratic Alliance Party, kinachojulikana kwa kifupi kama LINDA Party. Chama kingine ni Mwananchi Party.
Kwa mujibu wa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP), LINDA Party iliwasilisha jina hilo mnamo Novemba 15, 2024.
Majina mengine yaliyowasilishwa pamoja na ombi hilo ni Liberty National Democratic Party (LNDP) na Liberty Democratic Alliance (LDA). Tangu wakati huo, chama hicho kimeendelea kupitia mchakato wa usajili.
Viongozi wake ni Phenasio Thuku ambaye ni kiongozi wa chama, Karen Majanga anayehudumu kama Katibu Mkuu na Purity Ndanu ambaye ni Mweka Hazina wa Kitaifa.
Msajili huyo pia alithibitisha kuwa ombi la kuhifadhi jina la Mwananchi Party liliwasilishwa na Pius Onyango mwezi Julai 2026 na bado linaendelea kufanyiwa tathmini.
Bw Lorionokou alisisitiza kuwa chama ambacho jina lake limehifadhiwa hakiwezi kuchukuliwa au kubadilishwa na mtu mwingine bila kufuata taratibu za kisheria.
Katika mahojiano maalumu, Bw Lorionokou alisema wazi kuwa Linda Mwananchi Movement si chama cha kisiasa kilichosajiliwa.
“Linda Mwananchi Movement haijasajiliwa kama chama cha kisiasa. Ukweli ni kwamba si chama cha kisiasa kwa sasa,” alisema.
Kuhusu amri ya hivi majuzi ya Jopo la Mahakama la kutatua Migogoro ya Vyama vya Kisiasa (PPDT), msajili huyo alisema kuwa haijazuia michakato ya usajili ambayo tayari ilikuwa imeanza.
Alifafanua kuwa mahakama ilizuia tu ofisi yake kushughulikia maombi mapya yanayohusiana na jina la Linda Mwananchi kesi hiyo ikiendelea kusikilizwa.
“Hukumu hiyo ilizuia msajili kuhusu maombi mapya yanayohusiana na Linda au Mwananchi Movement. Maombi yaliyokuwa tayari katika mfumo yataendelea kushughulikiwa kama kawaida,” alisema.
Matamshi hayo yanamaanisha kuwa mchakato wa usajili wa LINDA Party na ombi la Mwananchi Party bado unaendelea.
Akizungumzia Pius Onyango, aliyewasilisha ombi la Mwananchi Party, Bw Lorionokou alisema ofisi yake haiwezi kuhusisha mtu huyo na mrengo wa kisiasa wa Seneta Sifuna au mwanasiasa mwingine yeyote bila ushahidi rasmi.
“Hatuwezi kuhusisha mwombaji na kundi lolote la kisiasa isipokuwa taarifa hizo ziwe sehemu ya maombi yaliyowasilishwa,” alisema.
Aidha, alikumbusha kuwa vyama vyote vinavyotaka kushiriki uchaguzi mkuu wa mwaka 2027 vinapaswa kuwa vimekamilisha usajili wao kufikia Oktoba 15, 2026.
Alisema usajili wa chama cha kisiasa si jambo rahisi kama wengi wanavyodhani.
Mbali na kuhifadhi jina, waombaji wanapaswa kuwasilisha katiba ya chama, itikadi zake, kuwa na makao makuu na ofisi katika kaunti 24, pamoja na kusajili angalau wanachama 1,000 katika kila mojawapo ya kaunti hizo.
Hata hivyo, hakufunga kabisa mlango kwa Linda Mwananchi Movement kufanikisha mchakato huo kabla ya muda uliowekwa, akisema kila kitu kitategemea jinsi watakavyotimiza masharti ya kisheria.
Msajili huyo pia alipuuza madai kutoka kwa baadhi ya viongozi wa upinzani kwamba ofisi yake inatatiza usajili wa vyama vinavyoonekana kuunga mkono upinzani.
Alisema tangu aingie afisini Oktoba 13, 2025, idadi ya vyama vilivyosajiliwa imeongezeka kutoka 91 hadi 99, jambo ambalo linaonyesha kuwa sheria zinatumika kwa usawa kwa wote.