Upinzani nao wazindua ‘Bajeti’ ya Mwananchi: ‘Tutafyeka nusu matumizi ya Ikulu’
MUUNGANO wa upinzani jana ulizindua kile ulichokiita Bajeti ya Wananchi na kuwataka wabunge kukataa Bajeti ya Serikali ya Sh4.82 trilioni pamoja na Mswada wa Fedha wa 2026, ukisema umeshindwa kushughulikia matatizo ya kiuchumi yanayowakabili Wakenya.
Ukiongozwa na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, upinzani ulidai serikali ya Rais William Ruto imeongeza mzigo wa madeni, ushuru na kupunguza fedha za huduma muhimu kama elimu na afya.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Kalonzo alisema bajeti ya serikali itaacha nakisi ya zaidi ya Sh1.1 trilioni ambayo italazimika kufadhiliwa kwa mikopo, jambo alilosema litaachia vizazi vijavyo mzigo mkubwa wa madeni.
Muungano huo unapendekeza kuongeza fedha za elimu kutoka Sh668.3 bilioni hadi Sh737.3 bilioni ili kufadhili kikamilifu elimu ya msingi, sekondari na sekondari msingi (JS).
Pia unapendekeza kupunguza matumizi ya usimamizi katika Wizara ya Elimu na kuelekeza fedha hizo kwa wanafunzi.
Katika sekta ya afya, upinzani umepanga kuongeza bajeti hadi Sh242.3 bilioni, kurejesha mpango wa Linda Mama na Edu Afya, pamoja na kuongeza fedha kuhakikisha hospitali za umma zina dawa na vifaa vya kutosha.
Waliahidi kufuta Ushuru wa Nyumba Nafuu na kupunguza baadhi ya ada zinazochangia kupanda kwa gharama ya maisha.
Aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua alisema serikali ya upinzani itafuta ushuru wa nyumba mara moja iwapo itashinda uchaguzi wa 2027.
Alionya pia Wakenya dhidi ya kununua nyumba za mpango wa nyumba nafuu au mali ya umma itakayouzwa kabla ya uchaguzi.
Ingawa upinzani hauna idadi ya kutosha ya wabunge kupitisha mapendekezo yake, uzinduzi wa Bajeti ya Wananchi unaonyesha mkakati wake wa kujijenga kama serikali mbadala na kuingia katika uchaguzi wa 2027 ukiwa na ajenda ya kupunguza gharama ya maisha na kuboresha huduma za umma.