Wafanyakazi wa KPA wahofia hatima yao baada ya tangazo la kukodisha huduma za kampuni
MAELFU ya Wafanyakazi wa Mamlaka ya Bandari Kenya (KPA) wameeleza wasiwasi wao kuhusu mikataba yao ya ajira baada ya kuchapishwa kwa zabuni ya kukodisha vifaa na huduma za operesheni.
Zabuni hiyo pia imetoa ombi la kutaka kuajiri wafanyakazi wenye tajriba maalum ya kazi.
Chini ya mkataba huo, KPA itahitaji jumla ya wafanyakazi 4,700 wenye ujuzi wa kutumia mashini mbalimbali na kutekeleza majukumu tofauti.
KPA ilitagaza mfumo wa mpito ambapo wafanyakazi ama watahudumu katika kampuni ya kibinafsi au kuajiriwa na KPA lakini kuhudumu katika taasisi nyingine.
Hii ni baada ya Mkurugenzi Mkuu, Kapteni William Ruto, kusema kwamba KPA itaathiriwa na Sheria mpya ya taasisi zinazomilikiwa na serikali.
Hata hivyo, wafanyakazi hao wanataka kujumuishwa kwenye swala hilo kwa ukamilifu wakitaka kujua hatma yao ya uajiri.
“Hatujui hatma yetu baada ya chapisho. Kwanza wasiwasi wetu mkubwa ni kuhusu maelezo katika zabuni hiyo ambayo inatoa maagizo kuhusu wafanyikazi wanaotakiwa bandarini,” alisema mfanyikazi mmoja ambaye alitaka jina lake libanwe.
Wafanyikazi wa KPA walisema huenda mpango huo ukawa sawia na zabuni ya Adani ambayo ilikuwa inapanga kukarabati uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta.
Hapo jana, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari ya Kenya (KPA), Capt William Ruto, aliwapongeza wafanyakazi kwa mchango wao katika kuboresha ufanisi wa bandari, akisema mafanikio ya Bandari ya Mombasa yametokana na mshikamano, ustahimilivu na kujitolea kwa wafanyakazi.
Akizungumza baada ya kukamilisha kikao cha siku mbili na wafanyakazi katika Bandari ya Mombasa, Capt Ruto alieleza kwa kina mpango wa mamlaka na kusisitiza dhamira ya usimamizi kuboresha maslahi ya wafanyakazi na utendakazi bora.
“Wafanyakazi wameimarisha shughli za bandari na kuifanya bandari hii kuendelea kuwa bandari bora zaindi katika ukanda huu. Uongozi wangu utaendelea kuipa kipaumbele maslahi ya wafanyakazi kwa sababu bila wafanyakazi hatuwezi kufanikisha malengo yetu,” alisema Capt Ruto bandarini.
Mwezi uliopita kwenye mahojiano na msemaji wa serikali, Bw Isaack Mwaura, alipinga madai kwamba bandari hiyo inabinafsishwa.
“Ni kama kumiliki ploti, jumba alafu nikukodishie nyumba uishi lakini nyumba na ploti hiyo ni yangu kwa hivyo hakuna lolote kuhusu ubinafsishaji. Tunataka msaada wa sekta ya kibinafsi ili kuimarisha shughli za bandari,” alifafanua Capt Ruto.
Alisema raslimali nyingi zilizoko bandarini hazitumiki kikamilifu sababu ya bajeti inayohitajika. Hata hivyo kujumuisha sekta ya kibinafsi itaimarisha shughli za bandari hiyo.
Kikao hicho pia kilitoa jukwaa kwa wafanyakazi kuzungumza moja kwa moja na usimamizi na kujadili mipango ya mamlaka hiyo.
Mwaka jana, Bandari ya Mombasa ilisajili jumla ya shehena ya mizigo ya tani milioni 45.45, ikilinganishwa na tani milioni 40.99 zilizorekodiwa mwaka wa 2024.
Vilevile, shehena ya makontena ilipita TEUs milioni 2.11, ikionyesha ukuaji endelevu wa shehena na ufanisi wa kiutendaji.
Kwa sasa wafanyikazi wa KPA wanataka kujua hatma yao baada ya kuchapishwa kwa zabuni hiyo. Kulingana na zabuni hiyo KPA itahitaji wafanyikazi.
Juhudi za Taifa Leo kuwasiliana na mwenyekiti wa chama cha makuli nchini Bw Sulman Owuor hazikufua dafu baada ya kutuma ujumbe kwamba yuko kwenye mkutano.