Kalonzo amtaka Rais Ruto kutoa orodha ya walioajiriwa hivi karibuni katika jeshi, polisi
VIONGOZI wa Wiper wamekosoa serikali kwa kile walichosema ni ugavi usio wa haki wa rasilimali, ajira na miradi ya maendeleo nchini.
Kiongozi wa chama hicho, Kalonzo Musyoka, amemtaka Rais William Ruto kutoa takwimu za Wakenya walioajiriwa hivi karibuni katika jeshi na polisi, akidai ajira hizo zimegawanywa kwa misingi ya kikabila.
Bw Musyoka pia alilaani kushambuliwa kwa viongozi, akimtaka Rais kuwajibika kwa matumizi ya nguvu kupita kiasi na ongezeko la ghasia za kisiasa.
Alitaja pia utata kuhusu zabuni ya sare mpya za polisi, madai ya “kuuzwa” kwa nafasi za walimu na mgogoro wa ardhi ya ekari 4,000 Taita Taveta.
Mbunge wa Matungulu, Mutinda Mule, alitishia kuishinikiza NCIC kuchunguza madai ya ajira za walimu kutolewa kupitia barua za wanasiasa.
Alimtaka Rais Ruto ndani ya siku saba kutoa idadi ya walioajiriwa kwa njia hiyo, la sivyo Wiper itaihusisha NCIC kupitia Bunge.
Madai hayo yanaibuka baada ya Spika Moses Wetang’ula kusema baadhi ya wabunge walipelekwa Ikulu kuchukua barua za ajira za walimu, ambazo baadaye ziliuzwa kwa hadi Sh400,000.