Habari

Alia kutengwa sababu ya kazi yake ya kupamba maiti

Na KALUME KAZUNGU August 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAHUDUMU wa wanaopamba miili ya waliokufa wameeleza changamoto wanazopitia katika jamii kutokana na unyanyapaa.

Bi Margaret Santa Thoya, 26, mkazi wa kijiji cha Muyeye kilicho Malindi, Kaunti ya Kilifi ambaye hutekeleza ulimbwende kwa waliokufa anasema kuwa urembeshaji anaoufanya husaidia kuboresha au kuipa maiti muonekano wa utulivu bila wengine kuogopa wanapoitazama.

Ni kupitia ujuzi wake ambapo hujipatia kati ya Sh1,500 na Sh7000 kwa kila kandarasi moja anayopata.

Malipo yake huyakadiria kulingana na hadhi au tabaka la familia husika, umri wa mwendazake na mfumo au namna ambayo familia husika itapendekeza mpendwa wao apambwe.

Amedumu katika kazi hiyo ya kupamba maiti kwa zaidi ya miaka minne sasa.

Alikamilisha masomo yake ya darasa la nane (KCPE) 2016 katika shule ya msingi ya Karima iliyoko viungani mwa mji wa Malindi.

Hakufaulu kuendeleza masomo yake ya juu kwani mama yake aliachwa mjane.

Aliwahi kufanya kazi katika saluni mjini Malindi, hivyo kupokea ujuzi wa kazi za urembo.

“Kuna siku ambapo niliraiwa na familia moja kwenda mochari Malindi kuwarembeshea mpendwa wao mwanamke aliyekuwa ameaga. Nilijikaza na kuitekeleza kazi hiyo vyema, hivyo nikalipwa fedha nzuri. Tangu hapo nikaamua kujiingiza mzimamzima kwenye nyanja hii ya kurembesha maiti,” akafichua Bi Santa.

Licha ya kujijengea jina kubwa katika kazi yake, kinachomsikitisha binti huyu ni jinsi baadhi ya wanajamii wanavyomtenga au kumsuta ilihali wengine wakiogopa kutangamana naye.

Analalamika kuwa miaka yote amekosa mume wa kumchumbia kwani wengi wao punde wanapomuona humtoroka huku wakimbandika majina ya ‘Maggie wa Mochari.’

“Sijapata mwanamume jasiri aliyewahi kunifuata kunichumbia. Wengi hawataki. Kuna ambao hata kuzungumza nami au kunisalimia ni shida.

Wakiniona kwa mbali utasikia wakinisuta eti ni yule ‘madam wa mochari.’ Wengine hutoroka au kunipisha njia kwa mbali wakihisi mimi ni nuksi maishani kwa maamuzi yangu ya kutangamana na kurembesha maiti,” akasema.

Tatizo lake hata hivyo haliwakumbi wanawake pekee wanaojihusisha na taaluma kama yake.

Bw Samson Karisa, mkazi wa mjini Kilifi alilazimika kuhamia mjini Malindi, karibu kilomita 61 kutoka kwao ilmuradi ajihusisha na biashara ya kurembesha maiti.

Anakiri kutekeleza jukumu lake kwa usiri mwingi kwani mamake mzazi, mkewe na wanawe wawili hawafahamu ni kazi gani hasa yeye hujihusisha nayo maishani kuleta mapato nyumbani.

Amekuwa akilipwa ili kurekebisha majeraha hasa endapo marehemu alipata ajali.

Yeye hutumia nta spesheli kuziba na kujenga upya sehemu zilizoharibika za mwili ili kuzipa mwonekano ufaao.

“Pia humvalisha nguo marehemu na kumweka katika jeneza kwenye pozi la kulala kwa amani, kuipanga mikono vizuri katika hali ya kawaida kifuani au tumboni,” akaeleza Bw Karisa.

Kutokana na kazi yake, jamii ya mjini Malindi tayari imembandika jina la ‘Karisa wa Kifa,’ Kiswahili Karisa wa Kifo.

Wataalamu wa saikolojia wanasema yale ambayo wawili hao wanapitia yanatokana na imani na desturi za jamii nyingi ambazo huamini chochote kinachohusiana na kifo huwa na mabaya.

Hata hivyo, jamii iliombwa itambue kuwa, kuna aina nyingi za kazi ambazo zinahusu masuala ya kifo.