Habari

Sifuna avamia ngome ya Raila

Na WAANDISHI WETU  August 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MAKABILIANO makali ya kisiasa yaliyoshuhudiwa Jumapili katika Kaunti ya Homa Bay yamefichua vita vinavyozidi kushika kasi vya kutaka kudhibiti ngome ya kisiasa ya marehemu Raila Odinga, huku makundi hasimu yakijiandaa kwa Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Linda Mwananchi, inayoongozwa na Gavana wa Siaya James Orengo na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, ilikaidi vizuizi vya barabarani, uvamizi na na hatimaye kuandaa mikutano Nyandiwa, Sindo na Homa Bay mjini.
Kuingia kwao katika eneo hilo kulionyesha wazi mtihani mkubwa kwa juhudi za Rais William Ruto na washirika wake kuendeleza ushawishi katika eneo la Luo Nyanza.
Eneo hilo lilimkataa katika uchaguzi wa 2022 na kumpigia kura mwanao marehemu Raila. Kwa sasa eneo hilo linangáng’aniwa na makundi mbalimbali ya kisiasa.
Upande mmoja ni kundi la ODM linalopinga kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto na sasa linaendesha shughuli zake chini ya vuguvugu la Linda Mwananchi.
Mrengo mwingine ni kambi inayounga mkono serikali, ambayo imekuwa ikitumia miradi ya maendeleo na teuzi serikalini kujipigia debe.
Homa Bay kwa miaka mingi imekuwa ngome kuu ya kisiasa ya Bw Odinga lakini sasa ni kitovu kinachongángániwa na mirengo hii miwili
Kufuatia kifo cha Bw Odinga mwaka jana, kilichoacha pengo kubwa la kisiasa, Homa Bay imekuwa eneo muhimu la kupimia ni nani atakayerithi ushawishi wake kisiasa.
Gavana Gladys Wanga, ambaye ametajwa kama mmoja wa viongozi wanaoweza kuchaguliwa kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto mnamo 2027, anakabiliwa na changamoto ya kulinda ngome ya jadi ya ODM.
Ana kibarua kuonyesha kuwa ushirikiano wa chama hicho na serikali ya Kenya Kwanza umeleta manufaa kwa eneo hilo.
Tangu aingie mamlakani, Rais Ruto ameongeza ushawishi wake wa kisiasa na miradi ya maendeleo katika Nyanza ya Waluo.
Serikali imetaja miradi kama kukamilishwa kwa Uwanja wa Raila Odinga, Gati ya Homa Bay, Soko la Samaki la Koginga, Ikulu ndogo , nyumba za gharama nafuu, Barabara ya Mzunguko ya Mfangano-Rusinga, ukarabati wa Chuo Kikuu cha Tom Mboya pamoja na ujenzi na uwekaji wa lami katika barabara mbalimbali.
Hata hivyo, Linda Mwananchi inatoa hoja tofauti ikisema barabara, viwanja na miradi mingine ya maendeleo haiwezi kuchukua nafasi ya uwajibikaji, haki za kidemokrasia na kuheshimu utawala wa sheria.
Bw Sifuna aliwaambia wakazi kuwa maendeleo hayafai kutumiwa kuwanyima haki za kikatiba na uongozi wenye uwajibikaji.
“Baba alituambia tuweke demokrasia, uhuru na kuheshimu utawala wa sheria mbele ya kila kitu, lakini baadhi ya watu wanataka kuwahadaa kwamba maendeleo yanatosha hata kama maana yake ni kumuua Albert Ojwang,” akasema, akirejelea mauaji ya mwalimu na mwanaharakati huyo kutoka Homa Bay.
Alisema serikali inayoheshimu utawala wa sheria haipaswi kuwa na tatizo la kuleta maendeleo.
“Kama Sifuna, kujenga barabara na viwanja si jambo gumu kwangu, lakini ninachowaahidi ni kwamba nitaheshimu utawala wa sheria, nitalinda haki zenu na sitawahi kuwaua watoto wenu,” akaongeza.
Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi pia alipinga hoja ya maendeleo, akisema eneo hilo halijastawi sana chini ya utawala wa sasa.
Bw Omondi alidai serikali imewekeza Sh50 bilioni katika eneo hilo, kiasi ambacho alisema ni sawa na gharama ya mradi mmoja mkubwa katika Bonde la Ufa.
Mbunge huyo pia aliishutumu serikali kwa kuchukua udhibiti wa kampuni za sukari katika eneo hilo, akitaja Miwani na Chemelil.
Gavana Orengo naye aligeuza mkutano huo kuwa jukwaa la kueleza ni nani anayepaswa kubeba urithi wa kisiasa wa Bw Odinga.
Alimshutumu Rais Ruto kwa kushindwa kushughulikia malalamishi ya muda mrefu ya Nyanza, yakiwemo mzozo wa Migingo, na kukosoa namna serikali ilivyoshughulikia maandamano na madai ya mauaji yaliyotekelezwa na polisi.
Kauli iliyovutia zaidi ilitolewa alipokuwa akijitaja kama mrithi wa kisiasa wa Bw Odinga.
“Hapa ndipo roho ya Raila ilipo, haikufa pamoja naye. Uongozi unachukuliwa, haupeanwi, na ndiyo maana mimi ndiye Raila aliyesalia,” akasema Bw Orengo.
Alitangaza kuwa Linda Mwananchi itaadhimisha mwaka mmoja tangu kifo cha Bw Odinga Oktoba 15, ambapo itaitaka serikali kutoa majibu kuhusu kifo chake.
Mkutano wa Homa Bay pia ulihudhuriwa na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi.
Bw Owino alimtaja Bw Orengo kama kiongozi anayeweza kuwa daraja kati ya viongozi wa upinzani ambao wamekuwa wakishindwa kuungana.
“Huyu ndiye mtu atakayewaleta viongozi hawa wote pamoja mezani na kuamua kuhusu kiongozi mmoja,” akasema.
Bw Natembeya na Bw Osotsi pia waliwahakikishia wafuasi kwamba miungano mipya ya upinzani haitavuruga uhusiano wa kihistoria kati ya jamii za Luo na Luhya.
Bw Natembeya alisema upinzani unahitaji kuunganisha zaidi uungwaji mkono wake Magharibi na Nyanza kuelekea uchaguzi wa 2027.
RIPOTI ZA GEORGE ODIWUOR, DOMNIC OMBOK na RUSHDIE OUDIA