• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 7:50 AM
Mgombeaji urais asusia mlo katika jela ya Tunisia

Mgombeaji urais asusia mlo katika jela ya Tunisia

Na MASHIRIKA

MMOJA wa wawaniaji wa urais nchini Tunisia, Nabil Karoui, ambaye alipigiwa upatu kushinda kiti hicho ameanza kususia chakula akitaka aruhusiwe kupiga kura kwenye uchaguzi mkuu wa Septemba 15.

Karoui, 56, anayemiliki kituo cha runinga cha Nessma TV alifungwa jela wiki tatu zilizopita kwa madai ya kutolipa kodi na ulanguzi na ‘utakatishaji’ wa pesa.

“Karoui alianza kususia chakula tangu Jumatano akitaka haki yake ya kupiga kura Jumapili,” wakili wake Ridha Belhadj alinukuliwa akisema.

Maafisa wa serikali hawakupatikana kutoa kauli yao kuhusu ripoti hiyo.

Mahakama ya Rufaa inatarajiwa kusikiliza ombi lake la kuachiliwa kwa dhamana akisubiri uamuzi wa mwisho.

Mfanyabiashara huyo anayepigiwa upatu kushinda urais alikamatwa baada ya kulaumiwa na baadhi ya wanasiasa na mashirika ya serikali kwa kutumia kituo chake kuvumisha azma yake ya kisiasa.

Kura za maoni nchini Tunisia zilionyesha Karoui akiongoza na kwamba kufungwa kwake kuliongeza umaarufu wake.

Wapinzani wake ni waziri mkuu Youssef Chahed, waziri wa ulinzi Abdelkarim Zbidi, aliyekuwa rais Moncef Marzouki, na Abdelfattah Mourou, naibu rais wa chama cha Kiislamu cha Ennahdha party.

Karoui alikamatwa siku ambayo serikali ilitangaza kuwa ilipiga marufuku vituo vitatu vya habari vilivyohusisha chake maarufu cha Nessma TV, kupeperusha habari za kampeni za urais kwa madai kwmba hazvikuwa na leseni.

Masaibu yake yalianza Mei baada ya kutangaza angegombea urais alipowekewa vikwazo na serikali.

Mnamo Juni 18, bunge lilibadilisha sheria ya uchaguzi ambayo ilimzuia Karoui kugombea kwa kumiliki kituo maarufu za televisheni ikisema alikitumia kujipigia debe.

Wadadisi wanasema mabadiliko hayo yalinuiwa kumzuia Karoui kugombea lakini Essebsi alikataa kutia sahihi sheria hiyo kabla ya kifo chake.

Karoui alikuwa msitari wa mbele kuunga Essebi kwenye uchaguzi wa 2014 na amekuwa hasimu mkuu wa waziri mkuu Chahed.

Bwanyenye huyo alikuwa ameeleza hofu yake akisema alikuwa akihujumiwa kwa sababu ya kuongezeka kwa umaarufu wake kabla ya uchaguzi ambao ulifuaia kifo cha Essebsi.

Tume ya uchaguzi ya Tunisia imeidhinisha wagombeaji 26 wakiwemo wanawake wawili na Marzouki.

Nchini Tunisia, rais husimamia masuala ya nchi za kigeni na ulinzi na hugawana mamlaka na waziri mkuu anayechaguliwa na bunge ambalo lina mamlaka ya masuala ya ndani.

Wapiga kura milioni saba wanatarajiwa kushiriki uchaguzi huo baada ya kampeni zilizohusu changamoto za kijamii na kiuchumi katika nchi hiyo ya Afrika Kaskazini.

Wafuasi wa Karoui wanamlaumu Chahed kwa kuchochea kukamatwa kwake, madai ambayo waziri huyo mkuu anakanusha.

You can share this post!

Sakaja: Ni muhimu kukubali Jubilee haiko kama zamani

Mwili wa bwanyenye Tob Cohen wapatikana katika tanki kwake...

adminleo