Kimataifa

Rais Museveni apumua kesi ya kupinga ushindi wake ikiondolewa

Na DAILY MONITOR February 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

 
RAIS wa Uganda, Yoweri Museveni sasa amepumua baada ya kesi iliyowasilishwa mahakamani kupinga ushindi wake katika uchaguzi mkuu wa Januari 15 kuondolewa.
Kesi hiyo ilikuwa imewasilishwa na mwaniaji wa urais Robert Kasibante wa chama cha NPP katika Mahakama ya Juu baada ya Museveni kutangazwa mshindi.
Katika notisi ambayo iliwasilishwa mahakamani, Kasibante aliomba kuondoa kesi hiyo pamoja na nyingine aliyowasilisha kukagua fomu zote za uchaguzi, mitambo iliyotumiwa kuwatambua wapigakura na vyombo vingine vilivyotumika katika uchaguzi huo.
Kasibante pia kwenye ombi lake aliirai mahakama kuwa kila upande ugharamike kivyake katika kesi hiyo na akaahidi kutii amri nyingine ambayo itatolewa na mahakama.
Ombi ambalo amewasilisha ya kuondoa kesi hiyo, hoja kuu ya Kasibante ni kwamba hataweza kulipa gharama ya ukaguzi na mahitaji ya kiufundi yatakayotumika.
“Kesi hii itahusisha utayarishaji wa data au takwimu nyingi na gharama ambayo itatumika ni ya juu mno,” akasema Kasibante kwenye ombi lake.
Alikiri kuwa kuchanganua data hiyo kutahitaji watalaamu huru kushirikishwa na pesa nyingi zitatumika kufanikisha hilo.
“Wataalamu hawa watahitajika kukusanya, kuandaa na kuchanganua data kuhusu uchaguzi maeneo yote nchini,” akaongeza akisema hana pesa ambazo zinaweza kugharimia kesi hiyo.
Kuondolewa kwa kesi hiyo kulitokea siku chache baada ya Majaji wa Mahakama ya Juu wakiongozwa na Jaji Mkuu Flavian Zeija kuandaa kikao na kubaini hoja nne kuu za kuangaziwa katika kesi hiyo.
Wakati wa kusikizwa kwa kesi mwezi uliopita, Kasibante aliwakilishwa na mawakili watatu, Rais Museveni naye alikuwa na mawakili wawili huku Tume ya Uchaguzi na Mipaka ya Uganda ikiwakilishwa na mawakili watatu pia.
Mwanasheria Mkuu Kiryowa Kiwanuka naye aliwakilisha Afisi ya Wakili wa Serikali.
Mahakama ilikuwa imeelezwa kuwa Kasibante alikuwa amewaorodhesha mashahidi wanne, tume ya uchaguzi ilikuwa na mashahidi sita akiwemo mwenyekiti Simon Byabakama na Katibu Richard Baabo.
Mahakama ya Juu bado haijatenga tarehe ya kusikizwa kwa ombi hilo jipya la Kasibante.
Iwapo mahakama itakubali, basi mipango ya kuapishwa kwa Rais Yoweri Museveni ambaye ameongoza Uganda tangu 1986 itaendelea.
Chini ya Katiba ya Uganda, kesi ya kupinga ushindi wa rais katika uchaguzi ikishawasilishwa, inaweza kuondolewa tu na mahakama.
Wiki jana, Museveni liedai kuwa mpinzani wake Robert Kyangulanyi maarufu kama Bobi Wine alichapisha kura milioni moja feki na nyingine milioni 1.7 kutoka Dubai ili kupata ushindi kwenye uchaguzi mkuu wa Januari 17.
Kiongozi huyo pia alisema kutumika kwa mfumo wa kielektroniki kwenye uchaguzi huo ndiko kulizuia njama ya upinzani kutumia njia ya udanganyifu katika kura hiyo.
Alidai kuwa kwa sasa hakuna upinzani Uganda kwa sababu wapigakura wameonyesha imani yao kwa kumpa kura kupitia NRM.
“Fahamu hakuna upinzani Uganda, hao wanaosema kunao wanajidanganya tu. Baada ya uchaguzi tuligundua walichapisha karatasi milioni moja za kupiga kura hapa barabara ya Nkuruma na milioni nyingine milioni 1.7 kutoka Dubai,” akasema Museveni.
Kiongozi alisifu matumizi ya mitambo ya kielektroniki ya kupiga kura akisema ilimwokoa kushindwa kwa njia ya udanganyifu na Kyangulanyi.