• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:07 PM
Rais wa zamani wa Pakistan ahukumiwa kifo

Rais wa zamani wa Pakistan ahukumiwa kifo

Na AFP

ALIYEKUWA rais wa zamani Pakistan Pervez Musharraf Jumanne alihukumiwa kifo na mahakama maalum kwa kosa la uhaini uliokithiri.

Musharraf ndiye kiongozi wa kwanza wa kijeshi kuwahi kufanyiwa mashtaka na kuhukumiwa kwa kosa la uhaini.

Kesi hiyo, pamoja na rundo la kesi nyinginezo zinazomkabili, iliwasilishwa dhidi yake mnamo 2013, baada ya kurejea kwake nchini Pakistan kutoka ukimbizini alimokaa kwa miaka minne, akinuia kugombea ubunge ili ‘kuliokoa’ taifa hilo lililojihami kwa silaha za nuklia.

Katika kesi hiyo, alikabiliwa na mashtaka ya kulemaza, kusambaratisha na kupuuzilia mbali katiba, kushinikiza hali ya hatari nchini humo mnamo Novemba 2007 pamoja na kuwazuilia majaji wa mahakama kuu zaidi nchini Pakistan.

Musharraf, aliyeondoka Pakistan punde baada ya kujiuzulu kama rais mnamo 2008, aliondoka taifa hilo kwa mara ya pili mnamo Machi 2016 kwa lengo la kusaka matibabu nchini Dubai. Alitangazwa kama mtoro katika kesi hiyo.

Musharraf alishtakiwa rasmi mnamo Machi 31, 2014, ambapo upande wa mashtaka ulikuwa umewasilisha ushahidi wote mbele ya mahakama spesheli mnamo Septemba mwaka huo pia.

Lakini mchakato wa kusikizwa kwa kesi hiyo ukaendelea.Korti spesheli, iliyoongozwa na Jaji Mkuu wa Mahakama Kuu ya Peshawar Waqar Ahmad Seth, ilikuwa imetangaza kuwa ingetoa hukumu yake hapo.

Hata hivyo, upande wa mashtaka unaowakilisha serikali kupitia kwa Wakili Ali Zia Bajwa, ulisema ulikuwa umewasilisha kesi tatu.

Kesi moja inaitaka mahakama kuwafanya watu watatu wakiwemo – aliyekuwa waziri mkuu Shaukat Aziz, aliyekuwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Juu Zaidi Abdul Hameed Dogar pamoja na aliyekuwa Waziri wa Sheria Zahid Hamid – kuwa washukiwa katika kesi hiyo.

“Tunataka kuwafanya washiriki na wandani wa Musharraf kuwa washukiwa vilevile. Ni muhimu kwamba kesi ya washukiwa wote ifanyike katika wakati mmoja,” alisema Bajwa, kulingana na vyombo vya habari nchini humo.

Wakati wa kusikizwa kwa kesi hiyo, wakili wa Musharraf, Raza Bashir pia aliomba muda wa kati ya siku 15 hadi 20 ili mteja wake aandikishe taarifa. “Musharraf anastahili haki ya kufanyiwa mashtaka kwa njia ya haki,” alisema.

You can share this post!

Mvua sasa kupungua siku 7 zijazo

Sonko kujibu mashtaka mapya Voi

adminleo