Kongamano la KAKAMA maadhimisho ya Kiswahili Burundi kutoa mwelekeo mpya
WANANCHI wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wametakiwa kushiriki kikamilifu ili kufikia malengo ya mwelekeo mpya ulioanzishwa na Kamisheni ya Kiswahili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (KAKAMA) katika kuhakikisha akiliunde inatumika kuleta maendeleo ya Kiswahili.
Kakama imeazimia kuanzisha mwelekeo huo mpya ili kuafikia mafanikio kupitia Kongamano la Kimataifa la Tatu ambalo linaanza kesho Jumapili Julai 5, 2026 na maadhimisho ya Siku Kiswahili Duniani Julai 7, ambapo kwa pamoja yanafanyika Bujumbura Burundi.
Akizungumza na waandishi wa habari, jijini Bujumbura wikendi, Katibu Mtendaji wa Kakama, Dk Caroline Asiimwe alisema kila nchi wanachama zinatakiwa kushiriki kikamilifu ili kufikisha azma ya Kakama kuleta maendeleo ya Kiswahili katika teknolojia ya akiliunde pamoja wingi lugha kama inavyosema kaulimbiu ya mwaka huu.
Amesema maeneo yanayotakiwa kutiliwa mkazo ni kwenye uwekezaji, ubunifu na ushirikiano.
Bi Asimwe ametoa wito uwekezaji zaidi ufanyike kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo kampuni za kuzalisha maudhui ya Kiswahili kwa kutumia akiliunde, kubuni mifumo mbalimbali na kuongeza ushirikiano wa kibunifu wa kikanda.
“Ninatoa wito kwa wana Afrika Mashariki kushiriki kwa namna mbalimbali ikiwemo kwenye uwekezaji, ubunifu na ushirikiano,” akasisitiza Dk Asiimwe.
Amesema watunga sera pia wanalojukumu kutumia fursa hiyo kwenye nchi wanachama kuhimiza sera zinazochochea matumizi ya teknolojia ya akili unde.
Dk Asiimwe amewakaribisha wana Afrika Mashariki kutoka kada mbalimbali kushiriki kongamano hilo kwa namna mbalimbali ikiwemo kufika kwenye mkutano na kufuatilia mitandaoni.
Amesema kongamano hilo linaenda sambamba na maadhimisho ya miaka 10 ya Kamisheni ya Kiswahili tangu kuazishwa kwake.
Amewataka wanajumuiya ya Afrika Mashariki kujivunia mafanikio mbalimbali yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa kamisheni hiyo.