Kabutha ahifadhi urais wa Netball Kenya huku viongozi wote wakichaguliwa bila kupingwa
RAIS wa Shirikisho la Netiboli Kenya (Netball Kenya), Immaculate Kabutha, amechaguliwa tena bila kupingwa baada ya wagombea wote kukosa wapinzani katika uchaguzi uliofanyika Jumamosi katika ukumbi wa Greenpark Terminus, Nairobi.
Uchaguzi huo uliosimamiwa na Bodi Huru ya Uchaguzi, haukuhitaji upigaji kura kwani wagombeaji wote waliowasilisha nyaraka zao walithibitishwa kuwa wametimiza masharti na hawakuwa na wapinzani.
Akizungumza baada ya kutangazwa mshindi, Kabutha alisema kuungwa mkono bila kupingwa ni ishara ya imani kubwa ambayo wajumbe wameweka kwa uongozi wa sasa, na akaahidi kuendelea kuimarisha mpira wa pete nchini.
“Hii ni siku kubwa kwetu. Wagombea wote wanane hawakupingwa, jambo ambalo limetufurahisha sana kwa sababu linaonyesha imani ambayo wajumbe wameonyesha kwetu. Hakuna aliyekuwa na shaka kuhusu uwezo wetu,” akatangaza.
Alisema kipaumbele cha uongozi mpya kitakuwa kuimarisha mchezo huo ili uwe na ushindani zaidi pamoja na kupanua njia za kuibua vipaji vya wachezaji kwa lengo la kuimarisha timu ya taifa.
“Tuna kazi nyingi mbele yetu. Tunahitaji kuuboresha mchezo ili uwe bora zaidi kuliko ulivyo sasa. Pia, tunahitaji kuwa na hazina kubwa ya wachezaji ili tuweze kujenga timu ya taifa yenye ushindani mkubwa,” akasema Kabutha.
Alieleza kuwa Kenya kwa sasa inakamats nafasi ya 21 duniani katika mchezo wa netiboli, mafanikio aliyosema yanatia fahari, huku akiongeza kuwa maandalizi tayari yameanza kwa michuano ya Afrika ya mwaka ujao ambayo itakuwa sehemu ya mchakato wa kufuzu kwa Kombe la Dunia la Netiboli la mwaka 2027 litakalofanyika Sydney, Australia.
“Tayari tumekamilisha uteuzi wa timu na tunaendelea na maandalizi ya kuhakikisha wachezaji wanaendelea na mazoezi,” akafichua.
Kabutha pia aliishukuru Serikali ya Kenya kwa kuendelea kuunga mkono maendeleo ya netiboli, akiwapongeza Waziri wa Michezo Salim Mvurya na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Elijah Mwangi kwa ushirikiano wao.
“Tunashukuru Serikali ya Kenya na Wizara ya Michezo kwa msaada wao mkubwa ambao umetuwezesha kufikia hatua tulipo sasa,” alisema.
Mjumbe wa Bodi Huru ya Uchaguzi, Eugene Sudi, alisema uchaguzi huo ulifanyika kwa kuzingatia Katiba ya Kenya, Sheria ya Michezo pamoja na katiba na kanuni za Netball Kenya.
“Wagombea waliwasilisha nyaraka zao kwa ajili ya uhakiki na wote walibainika kuwa wamekidhi vigezo vya kugombea nafasi husika. Kwa kuwa hawakuwa na wapinzani, hakukuwa na haja ya kupiga kura. Tulichofanya ni kuwathibitisha rasmi kuwa wamechaguliwa,” akasema Sudi.
Aliongeza kuwa shughuli nzima iliendeshwa kwa utaratibu bila changamoto zozote na kwamba viongozi waliochaguliwa wanakidhi matakwa yote ya sheria kuhusu uongozi wa mashirikisho ya michezo.
Msajili wa Michezo, Rose Wasike, pamoja na maafisa kutoka Wizara ya Michezo na Afisa Mtendaji wa Baraza la Kitaifa la Michezo Kenya (KNSC), James Akama, walihudhuria uchaguzi huo. Maafisa wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) walisimamia zoezi hilo.
Akizungumza na viongozi wapya, Wasike aliwakumbusha kuwa nafasi walizopewa ni dhamana ya kuwatumikia wanachama na si mali yao binafsi.
“Mmechaguliwa kuhudumu. Hili si shirika lenu binafsi. Kuweni wawajibikaji,” akashauri.