Habari

Mgomo: Masharti makali wanafunzi wakirejea shuleni

Na WAANDISHI WETU  June 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BAADA ya wimbi la migomo, wanafunzi wanatarajiwa kuerejea shuleni huku wazazi wakikabiliwa na hali ngumu ya kulipia mali ambayo iliharibiwa.

Wanafunzi wa Shule ya Upili ya Mangú (Kaunti ya Kiambu) na ile ya upili ya Chasimba (Kilifi) watalipa Sh1,000 kila mmoja.

Wenzao kutoka shule ya wasichana ya Moi Lanet na ile ya wavulana wa Kakamaga nao watalazimika kulipa karo yote kabla ya kuruhusiwa shuleni.

Katika Shule ya Wasichana ya Utumishi, hali itakuwa ngumu zaidi kisaikolojia baada ya wanafunzi 16 kuangamia kutokana na kisa cha moto shuleni humo.

Wanafunzi itabidi wapitie hali ngumu, baadhi wakirejea wakiwa na makovu ya moto huo.

 

Kote nchini, wazazi, wasimamizi wa shule, wakuu wa elimu hata hivyo wanajiuliza swali mmoja, mbona wanafunzi wanashiriki mgomo.

Wiki jana Waziri wa Elimu, Julius Ogamba, alifichua kuwa shule 204 ziliathirika na mgomo huo japo alisema zinawakilisha asilimia mbili pekee ya shule zote kote nchini.

Baada ya migomo angalau shughuli za masomo zimerejea katika zaidi ya shule 59 huku mamlaka husika zikilenga kurejesha hali ya kawaida shuleni.

Katika Shule ya Upili ya Agoro Sare, Mwalimu Mkuu Isack Okeyo alisema baadhi ya wanafunzi walioteketeza bweni walifanya hivyo kutokana na wimbi la mgomo ambalo lilikuwa likishuhudiwa kwingine.

“Washukiwa wawili walisema walifanya hivyo kutokana na yaliyokuwa yakiendelea katika shule nyinginezo. Bado hatujapokea ripoti ya kutathmini kiwango cha uharibifu ili tujue kila mwanafunzi atalipa ngapi,” akaambia Taifa Leo.

Washikadau sasa wanalaumu mitandao ya kijamii, simu kama zilizosababisha kuenea kwa visa vya kuteketeza shule moto.

Katika Kaunti ya Siaya, Mahakama Kuu ililazimika kuingilia kati baada ya usimamizi wa Shule ya Upili ya Ambira kuwataka wazazi walipe Sh33,000 kwa kila mwanafunzi.

Pesa hizo zilikuwa za kufanya ukarabati majengo yaliyoteketezwa mnamo Mei 18.

Shule hiyo ilikadiria uharibifu huo ni wa Sh50 milioni na kuamrisha wazazi wachangie kabla ya wanafunzi kurejelea masomo.

Wazazi walipinga uamuzi huo kortini.

Kupitia wakili wao John Kihara, wazazi walishutumu usimamizi wa shule kwa kukimya huku baadhi ya viranja wakiwalawiti vijana wadogo.

Katika Shule ya Upili ya Kakamega, wanafunzi waliamrishwa wamalize karo ya muhula wa pili kabla ya kurejea ikizingatiwa bweni liliteketezwa.

Mmoja wa wanafunzi alisema kulikuwa na taharuki zaidi ya wiki moja kabla ya moto huo.

“Haikuwa tu suala la kuenda nyumbani kwa sababu tulikuwa tumelalamika chakula kilikuwa kidogo lakini usimamizi wa shule haukuwa ukitusikiza. Pia huwa tunatazama runinga na kuna baadhi ya wanafunzi ambao wana simu,” akasema.