Makosa ya Uhuru yagharimu Wakenya Sh175 milioni
UAMUZI wa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta mwaka 2020 kukataa kuteua majaji 41, licha ya amri za mahakama kumtaka afanye hivyo, umegeuka kuwa mzigo kwa walipa ushuru ambao sasa wanalazimika kulipa mamilioni ya fedha kufidia waliowasilisha kesi mahakamani.
Wakati huo, Rais Kenyatta alinukuu ripoti ya kijasusi iliyodai kuwa baadhi ya waliopendekezwa hawakufaa kuhudumu kama majaji.
Hata hivyo, hadi leo ripoti hiyo na ujumbe wake umeendelea kuwa siri inayojulikana na watu wachache serikalini.
Mmoja wa waliopendekezwa, Harrison Okeche, alifariki Oktoba 2020, miezi mitatu tu baada ya Tume ya Huduma kwa Mahakama (JSC) kuwasilisha jina lake kwa rais ili ateuliwe kuhudumu katika Mahakama ya Mazingira na Ardhi.
Sasa imebainika kuwa hatua hiyo ilikuwa kosa la kiutendaji, kwani walipa ushuru ndio wanaobeba gharama ya maamuzi hayo.
Wiki iliyopita, kesi ya majaji 22 waliopendekezwa kuhudumu katika Mahakama ya Mazingira na Ardhi ilifaulu, na kufanya jumla ya fidia kufikia Sh175 milioni.
Kiasi hicho hakijumuishi gharama za mawakili ambazo pia zitalipwa na walipa ushuru kwa waliowasilisha kesi na kushinda.
Majaji hao 22 walitunukiwa jumla ya Sh55 milioni kwa kukiukwa kwa haki zao baada ya kusubiri kwa miezi 21 kabla ya kuapishwa.
Mnamo Oktoba 2024, majaji wengine sita—wanne waliopendekezwa kwa Mahakama ya Rufaa na wawili kwa Mahakama ya Mazingira na Ardhi, walishtaki Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na kutunukiwa Sh120 milioni baada ya kusubiri kwa takriban miaka mitatu.
Kesi hizo zimefaulu kwa misingi kadhaa, mojawapo ikiwa ni kanuni ya “matarajio halali”.
Sheria hairuhusu Rais kupuuza mapendekezo ya Tume ya Huduma za Mahakama katika uteuzi wa majaji.
Kwa hivyo, matarajio ya majaji hao kwamba wangeteuliwa rasmi kupitia notisi ya gazeti la serikali na kuapishwa yalikuwa halali kisheria. Kusubiri kwa miezi 21 kulionekana kama ukiukaji wa haki zao.