Matiang’i aonya dhidi ya kuiba kura Upinzani ukiahidi kuungana
VINARA wa Muungano wa Upinzani wamemuonya Rais William Ruto dhidi ya kujihusisha na mchezo wowote mchafu katika uchaguzi mkuu wa 2027, wakisema hawataruhusu kura zao kuibwa.
Viongozi hao, ambao wanajitahidi kusuka muungano kuelekea uchaguzi ujao, walirejelea wasiwasi kuhusu teknolojia ya uchaguzi iliyotumika katika Uchaguzi Mkuu wa 2022.
Walilalamikia hasa mfumo uliouzwa na kusimamiwa na kampuni ya Smartmatic iliyoibuka mshindi wa zabuni ya kuendesha Mfumo wa Usimamizi wa Uchaguzi wa Kenya (KIEMS), wakisema haupaswi kutumika katika uchaguzi ujao.
“Nililinda mtihani hadi ukakosa kuibwa. Hamtaweza kuiba kura zetu,” alisema naibu kiongozi wa chama cha Jubilee, Dkt Fred Matiang’i akizungumza jana, Jumapili, Februari 22 katika kanisa la PCEA Utawala, Nairobi.
Waziri huyo wa zamani wa usalama wa ndani alionya serikali dhidi ya kutumia wahuni kuvuruga mikutano ya upinzani.
Kulingana na kiongozi wa chama cha DCP, Rigathi Gachagua, muungano wa upinzani umeweka presha kwa serikali.
“Huyu jamaa tumemsukuma kwa kona,” alisema Gachagua, akimrejelea Rais Ruto, na kuwataka wafuasi wao kutokuwa na wasiwasi.
Viongozi wa upinzani walisawiri muungano wao wa kisiasa kama “vita vya kimaadili dhidi ya utawala uliofeli.”
“Adui wa Wakenya ni mmoja,” alisema kiongozi wa Chama cha People’s Liberation Party Martha Karua.
“Tujitokeze kuungana ili kujikomboa na kuondoa utawala mbaya.”
Kauli yake ilisitiliwa mkazo na kiongozi wa DAP-K Eugene Wamalwa ambaye alisema, “Tunaumizwa na utawala mbaya wa Ruto,” huku umati ukishangilia.
Kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka alikosoa mfumo wa Smartmatic katika uchaguzi wa 2022. “Hatutaruhusu Smartmatic kutumika katika uchaguzi ujao,” alisema Musyoka., akiongeza kuwa “wakati huu, hatutaruhusu kura kuibwa.”
Vinara hao wa upinzani, ambao walisema wanaweka kando tamaa zao binafsi ili kuungana, walieleza umati huo kwamba wamejizatiti kufanya kazi pamoja kumshinda Rais Ruto katika uchaguzi wa 2027.