Habari

Omtatah: Muungano wa Otuoma, Ojamoong haunibabaishi

Na CECIL ODONGO June 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SENATA wa Busia, Okiya Omtatah, amesema kuwa hateteshwi kisiasa na yanayoendelea katika Kaunti ya Busia huku akifichua kuwa kamati aliyobuni kutathmini ufaafu wake wa kuwania urais itakamilisha kazi yake mwezi huu na kisha kuizindua mapema Julai.

Bw Omtatah anashikilia kuwa kampeni za urais 2027 zinahitaji maandalizi makubwa ndiyo maana alikuwa makini kuwa na jukwaa imara ambalo litawapa maslahi ya Wakenya mstari wa mbele.

Seneta huyo kwa sasa ana maamuzi magumu kufanya kisiasa hasa baada ya Gavana wa kwanza wa Busia, Sospeter Ojamoong, kutangaza kuwa atagombea useneta Busia mnamo 2027.

Bw Ojamoong tayari amepata uungwaji mkono kutoka kwa Gavana wa sasa wa Busia Paul Otuoma ambaye analenga kutetetea kiti chake kupitia ODM.

Mnamo November 2024, Bw Omtatah alibuni kamati ya watu 10 kutathmini ufaafu wake wa kuwania urais mnamo 2027.

Kamati hiyo inaongozwa na Mary Kathomi Riungu na naibu wake Charles Okabaiku ambao wote sasa wanatarajiwa kukamilisha kazi yao siku chache zijazo kisha ripoti yao izinduliwe na seneta huyo mapema Julai.

“Ripoti inaelekea kukamilishwa na nitakuwa naipokea kisha tuizindue rasmi mapema Julai. Masuala yote yatakuwa yameangaziwa na hapo ndipo nitaamua iwapo nitawania urais au kurudi Busia kutetea kiti cha useneta wa Busia,” akasema Bw Omtatah kwenye mahojiano na Taifa Leo.

Baada ya maandamano ya Gen Z 2024, Bw Omtatah alikuwa kati ya viongozi ambao waliojizolea umaarufu kama ambao wangemtoa Rais Ruto kijasho katika uchaguzi mkuu wa 2027.

Hii ilitokana na uanaharakati wa kuwatetea vijana ambao walikuwa wamekamatwa na pia alikuwa mkosoaji mkali wa serikali hasa kuhusu uvunjanji wa haki.

Hata hivyo, kwenye ripoti ya TIFA iliyotolewa mwezi uliopita, hakuwa kati ya wale ambao waliorodheshwa kuwa wapo pazuri kumbwaga Rais Ruto.

Umaarufu ambao alikuwa nao akibuni kamati ya kutathmini ubora wake wa kuwania urais unaonekana kuyeyuka na kuwaendea Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino.

“Huwa sipigi kelele kwenye mazishi kama wanasiasa wengine ndio nijulikane nipo kwa sababu kazi yangu ni kutetea maslahi ya watu wa Busia na Wakenya kwenye Seneti. Siasa zangu huwa zinaongozwa na mikakati badala ya hadaa tupu,” akaongeza.

Seneta huyo alisema kuwa hatasita kuwania urais iwapo matokeo ya kamati aliyobuni itamshauri hivyo kwa sababu vigezo vyote vitakuwa vimeangaziwa.

“Hawa watu ambao wapo kinyangányironi kwa sasa hawana agenda ila lengo lao tu ni kumwondoa Rais Ruto mamlakani. Hoja si kumtoa Ruto kisha nafasi yake ichukuliwe na watu hawa ambao wanalenga kuendeleza uongozi mbaya tu kama yeye.

“Kile muhimu ni kwamba tuwe na rais ambaye atajali maslahi ya Wakenya si tu kuondoa utawala wa sasa kisha wanaoingia nao waendeleze maovu ambayo tumekuwa tukiyaona nchini,” akasema Bw Omtatah.

Kiongozi huyo alionyesha imani kuwa iwapo atawania urais ana uwezo wa kumbwaga Rais Ruto.

Hata hivyo, alisema hawezi kujiunga na mrengo wa Muungano wa Umoja wa Upinzani au Linda Mwananchi akisema mirengo hiyo haina agenda ya kutimiza maslahi ya Wakenya ila tu kumwondoa Rais Ruto.

“Wanasimamia nini kando na kumwondoa Rais Ruto madarakani? Hadi sasa sijaona chochote kipya ambacho wanaleta au watakachokifanya tofauti na Rais Ruto,’’ akasema.

Hatua ya Bw Otuoma kumuunga Bw Ojamoong inaonekana kutomtia seneta huyu wasiwasi akisema kuwa yupo tayari kupambana naye debeni iwapo hatawania urais.

“Ojamoong ana haki ya kuwania kiti chochote kile anachotaka ila sote tunafahamu kuwa katika muhula wa miaka 10 aliyoiongoza Busia hakuna chochote ambacho kilifanyika cha maana kimaendeleo. Sasa wameungana na Gavana Otuoma ambaye pia serikali yake imetawaliwa na ufisadi wakidai kuwa nimeenda kortini kuzuia miradi isilitwe Busia, walete huo ushahidi wao,” akasema.