Habari

Ni kuhangaika huku bei ya mafuta ikikadiriwa kuendelea kupanda zaidi

Na JOHN MUTUA May 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KUNA Kuna uwezekano wa bei ya dizeli kupanda zaidi hadi Sh300 kwa lita katika miezi michache ijayo kufuatia tahadhari kuhusu kupanda kwa gharama ya usafirishaji wa mafuta pamoja na kupungua kwa fedha katika hazina ya ruzuku ya mafuta.
Maafisa wa serikali na wauzaji wa mafuta wanaamini kuwa bei ya mafuta nchini itaendelea kupanda huku mzozo katika Mashariki ya Kati ukiendelea na fedha katika Hazina Maendeleo ya Petroli zikizidi kupungua.
Mamlaka ya Kuthibiti Kawi na Petroli (EPRA) Alhamisi iliongeza bei ya mafuta kwa hadi asilimia 23.5, na kusababisha bei ya dizeli kupanda hadi Sh242.92 kwa lita baada ya kuongeza bei hiyo kwa asilimia 24.2 mwezi uliopita.
Ongezeko hilo limechochewa na uhaba wa mafuta ghafi duniani pamoja na kupanda kwa gharama ya kawi kutokana na vita vinavyoendelea Mashariki ya Kati.
Bila ruzuku iliyotolewa katika miezi ya Aprili na Mei, dizeli ingeuzwa kwa Sh279.58 kwa lita huku petroli ikiuzwa kwa Sh218.59 badala ya Sh214.25 ya sasa.
Bei ya mafuta ya taa nayo ingepanda hadi Sh333.48 kwa lita kutoka Sh152.78 ya sasa. “Bila ruzuku na ikiwa Mkondo Bahari wa Hormuz utaendelea kufungwa, kuna uwezekano mkubwa wa bei ya dizeli kuvuka Sh300 kwa lita katika siku zijazo,” alisema afisa mmoja wa ngazi ya juu katika Wizara ya Kawi ambaye hakutaka jina lake litajwe kwa hofu ya kuchukuliwa hatua na serikali.
Kupanda kwa bei ya mafuta kunatarajiwa kuongeza mfumuko wa bei na kusababisha ongezeko la gharama katika sekta mbalimbali za uchumi.
Mafuta yana mchango mkubwa katika mfumuko wa bei nchini Kenya kwa sababu taifa hili hutegemea dizeli katika usafiri, uzalishaji wa umeme na kilimo, huku mafuta ya taa yakitumiwa na familia nyingi kupikia na kwa mwangaza.
Takwimu kutoka Shirika la Kitaifa la Takwimu zinaonyesha kuwa, mfumuko wa bei uliongezeka hadi asilimia 5.6 mnamo Aprili kutoka asilimia 4.4 mwezi uliotangulia, kiwango kikubwa zaidi katika kipindi cha miaka saba.
Hazina inayotumiwa kulinda Wakenya dhidi ya bei ya juu ya mafuta imeanza kupungua fedha huku serikali ikijitahidi kufidia kampuni za mafuta kwa kuuza petroli, dizeli na mafuta ya taa kwa bei ya chini kuliko ya soko.
Hali hiyo imeacha deni la zaidi ya Sh20 bilioni. Tatizo hilo limeongezeka baada ya kampuni ya mafuta ya Saudi Arabia, Saudi Aramco, kuonya kuwa vita kati ya Amerika na Iran vimezilazimisha kubadilisha masharti ya mpango wa serikali kwa serikali (G-to-G) na kwamba, mafuta yatakayowasili Mei, Juni na Julai yatauzwa kwa bei ya juu zaidi.
Kampuni ya Aramco Trading Fujairah (ATF) iliandikia Kenya ikisema kuwa imekuwa ikinunua mafuta kutoka maeneo mengine kwa gharama kubwa zaidi na gharama hiyo itahamishiwa kwa Kenya.
“Hali ya sasa ya vita vya Iran imetulazimu kupata mafuta kutoka maeneo mbadala ili kutimiza wajibu wetu wa kimkataba. Kupata mafuta kutoka maeneo hayo kutachelewesha usafirishaji na pamoja na mazingira ya sasa ya bei ya juu, itaongeza moja kwa moja gharama ya mafuta tunayopata,” ilisema Aramco katika taarifa yake kwa Kenya.
Kampuni hiyo ilisema hali hiyo ni tahadhari chini ya makubaliano ya msingi ya kandarasi na ikaomba bei ya usafirishaji wa mafuta ibadilishwe.
Kenya huagiza karibu mafuta yake yote kutoka Mashariki ya Kati kupitia mikataba ya serikali kwa serikali na kampuni za Ghuba kama Saudi Aramco, ADNOC Global Trading Ltd ya Abu Dhabi na Emirates National Oil Company Singapore Ltd.
Baadhi ya vipengele vya mikataba hiyo vinatoa nafasi kwa Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu kuongeza bei ya mafuta yanayouzwa kwa Kenya iwapo kutatokea mabadiliko makubwa yanayoathiri utekelezaji wa kandarasi.
Mabadiliko hayo yanaweza kujumuisha vita, kufungwa kwa njia za usafirishaji au ongezeko kubwa la gharama za kupata mafuta.
Vita vya Iran sasa vimepatia mataifa hayo ya Ghuba nafasi ya kuongeza bei ili kujilinda dhidi ya gharama kubwa ya kupata mafuta kutoka mataifa mengine pamoja na kupanda kwa gharama ya usafirishaji na bima.
Imebainika pia kuwa, migogoro ya kimataifa ni miongoni mwa sababu zinazoweza kupatia mataifa hayo uwezo wa kuondoa viwango vya juu vya bei vilivyowekwa katika mikataba na kuongeza gharama ya mafuta.
Aramco pia imeonya kuwa, akiba ya dizeli, petroli na mafuta ya ndege duniani inaweza kushuka hadi viwango vya hatari katika miezi ya kiangazi kati ya Juni na Agosti ikiwa Mkondo wa Hormuz utaendelea kufungwa.
Wachambuzi wa kimataifa wameonya kuwa, bei ya mafuta na gesi haitashuka hivi karibuni hata kama vita vya Iran vitaisha kutokana na shinikizo la upungufu wa mafuta na ushindani mkubwa katika soko la dunia.
Kupitia mfumo wa ruzuku, kampuni za mafuta huendelea kuuza mafuta kwa bei iliyotangazwa na EPRA huku serikali ikizilipa tofauti ya gharama kutoka Hazina ya Ushuru wa Maendeleo ya Petroli.
Ushuru huo hukusanywa kwa kiwango cha Sh5.40 kwa kila lita ya petroli na dizeli. Kiwango hicho kiliongezwa kutoka Sh0.40 kwa lita kuanzia Julai 2021 huku serikali ikijaribu kuongeza fedha za ruzuku ya mafuta.
Kwa sasa, serikali inadaiwa Sh6.042 bilioni na kampuni za mafuta kutokana na ruzuku iliyotolewa katika mwezi uliomalizika Mei 14.
Isitoshe, kuna deni lililothibitishwa lakini halijalipwa la Sh1.7 bilioni pamoja na Sh9 bilioni nyingine zinazongoja kuthibitishwa