OneTam: Upinzani wasisitiza umeungana licha ya mikutano tofauti
WASIWASI wa kuwepo kwa mvutano mpya umeibuka ndani ya muungano wa upinzani huku kampeni sambamba za viongozi wakuu zikizua maswali mazito kuhusu mshikamano, uratibu na mkakati wa pamoja kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Awali, muungano huo uliwasilishwa kama jukwaa imara na lenye nidhamu la kumtoa jasho Rais William Ruto, lakini sasa unaonekana kukumbwa na migawanyiko ya ndani, huku makundi mbalimbali yakifanya shughuli zake kivyake bila mwongozo wa pamoja.
Kundi moja linaongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kwa ushirikiano na kiongozi wa Wiper Democratic Movement Kalonzo Musyoka.
Wawili hao wamekuwa wakifanya ziara za pamoja na viongozi wengine kama Eugene Wamalwa wa DAP-K na Justin Muturi wa DP, wakilenga kuimarisha uwepo wao mashinani.
Kwa upande mwingine, mgombea urais wa Jubilee Fred Matiang’i, kiongozi wa PLP Martha Karua na Peter Munya wa PNU wamechagua kuendesha kampeni zao kivyama katika maeneo tofauti.
Hatua hii imezua mjadala kuhusu uwezekano wa kuwepo kwa mpasuko ndani ya muungano huo, huku kila kundi likionekana kujipanga kivyake kisiasa.
Katika siku za hivi karibuni, kambi ya Gachagua na Kalonzo imekuwa ikizuru maeneo ya Lower Eastern na Pwani, huku Karua akifanya mikutano Kirinyaga na Nyeri, na Matiang’i akijikita Nakuru na Kisii. Hali hii ya kampeni sambamba imeibua maswali kuhusu iwapo kweli kuna mkakati wa pamoja au kila kiongozi anajenga msingi wake binafsi kabla ya makubaliano ya mwisho.
Vyanzo vya ndani ya muungano vinaeleza kuwa kuna changamoto za mawasiliano na uratibu, ambapo baadhi ya viongozi hawashirikishwi mapema katika maamuzi muhimu. Hali hii husababisha migongano ya ratiba na hata hisia za kutengwa kwa baadhi ya viongozi.
Baadhi ya wadadisi pia wanakosoa mtindo wa uongozi ndani ya baadhi ya kambi wakisema unazua malalamishi ya udhibiti wa maamuzi na ukosefu wa ushirikishaji.
Hata hivyo, Martha Karua amepuuzilia mbali madai ya mgawanyiko, akisema kinachoonekana kama ushindani ni sehemu ya mchakato wa kidemokrasia wa kuwapa viongozi nafasi ya kujitambulisha kwa Wakenya.
Amesisitiza kuwa mwishowe vinara hao wataungana na kuwasilisha mgombea mmoja kupitia mchakato wa haki.
Msemaji wa muungano huo Mukhisa Kituyi naye amesema mikutano ya pamoja na ya kivyama ni sehemu ya kalenda ya kawaida ya kisiasa, akiongeza kuwa hali hiyo haipaswi kufasiriwa moja kwa moja kama mgawanyiko.
Wachambuzi wa siasa wanaonya kuwa licha ya maelezo hayo, picha inayoonekana hadharani ni muhimu kisiasa.
Mdadisi wa siasa Dismas Mokua anaonya kuwa iwapo hali hii haitashughulikiwa mapema, muungano huo unaweza kudhoofishwa na migogoro ya ndani badala ya kujikita katika kukabili mpinzani wake mkuu.
Hata hivyo, baadhi ya viongozi kama Cleophas Malala na Wamalwa wanasisitiza kuwa kampeni sambamba ni mkakati wa makusudi unaolenga kufikia maeneo mengi kwa muda mfupi.
Kiini cha mvutano huu kinasalia kuwa suala la nani atakuwa mgombea urais wa muungano huo. Kambi ya Gachagua inapendelea makubaliano ya viongozi wakuu, huku upande wa Matiang’i ukisisitiza mchakato wa kisayansi unaozingatia kura za maoni na ushawishi kitaifa.
Kutokuwepo kwa mfumo rasmi wa kufanya maamuzi, pamoja na kucheleweshwa kwa mkutano muhimu uliotarajiwa kufanyika Naivasha, kumeacha muungano huo katika hali ya sintofahamu. Bila suluhu ya haraka, muungano huo unaweza kupoteza mwelekeo hata kabla ya kuanza rasmi kwa kinyang’anyiro cha 2027.