Habari

Sitakupigia magoti Mlima Kenya, Ruto aambia Gachagua

Na MWANGI MUIRURI April 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto amemjibu vikali aliyekuwa Naibu wake na kiongozi wa Democracy for the Citizens Party Rigathi Gachagua, akisema hatompigia magoti ili kupata kura za Mlima Kenya.
Akizungumza Jumamosi katika Kaunti ya Murang’a wakati akihitimisha ziara ya siku mbili, Rais Ruto alisema uhusiano wake na wananchi hautategemea vitisho vya kisiasa.
“Nitamnyenyekea tu kwa mpiga kura. Wewe si Mungu. Magoti yangu yako kwa Mungu wangu; kujisalimisha ni kwa wananchi, na si lazima mtu apate kura. Watu wataamua kwa njia yoyote. Hakuna kura za Mlima Kenya unazobeba mfukoni,” alisema Rais.
Katika ziara hiyo, Rais alitembelea maeneo ya Maragua, Kigumo, Kandara na Gatanga, akikagua ujenzi wa masoko ya Ciumbu, Sabasaba, Kangari na Kabati, pamoja na barabara ya Kangari–Gichagi-ini-Githumu–Gacharage.
Pia alizindua kisima cha maji Kangari na kukabidhi vifaa vya maziwa kwa vyama vya ushirika.
Rais Ruto, aliyesikika akiwa na hasira, alimshutumu Gachagua kwa siasa za matusi na chuki, akisema analenga kudhibiti maamuzi ya wananchi.
“Anataka kuchagua muziki tunaosikiliza. Anataka kutuchagulia kanisa la kwenda, na viongozi tunaopaswa kushirikiana nao. Wanataka niwe mfanyakazi wao wa nyumbani, siwezi,” alisema.
Aidha alisema wapinzani wake hauna ajenda wala dira, akisisitiza kuwa serikali yake inaendelea kutekeleza ahadi alizotoa mwaka wa 2022 kupitia ajenda ya uchumi wa chini kwenda juu.
Bw Gachagua amesema kuwa Rais Ruto yuko katika wakati mgumu kisiasa, akimlaumu kwa kudanganya Mlima Kenya.
“Rais amekwama kwenye udanganyifu wake. Nilimwonya asisumbue Mlima. Alidharau. Acha avune alichopanda,” alisema akiwa Mombasa.
Gachagua ameanzisha kampeni inayoitwa “Fagia wasaliti” akilenga kuhakikisha viongozi wanaomuunga mkono Rais hawachaguliwi tena mwaka 2027, huku akidai atapunguza kura za Ruto Mlima Kenya hadi chini ya asilimia tano.
Katika ziara yake Rais Ruto pia alionekana kumtetea Naibu Rais Kithure Kindiki, akimtaja kama kiongozi mtulivu na mwenye uwezo wa kupanga mikakati ya kisiasa.
“Mlima Kenya una historia ya Mwai Kibaki kama kielelezo cha siasa za maendeleo. Tujifunze kufanya siasa za maendeleo,” alisema Kindiki.
Naye Kiongozi wa Wengi Bungeni Kimani Ichung’wah alimlaumu Gachagua kwa siasa za matusi na vitisho, akisema: “Hatuwezi kumwinamia mtu yeyote. Tutalinda heshima ya wananchi.”
Hata hivyo, ziara hiyo ilikumbwa na mvutano, kelele na maandamano ya vijana walioteketeza vifaa vya chama cha UDA, ishara ya mabadiliko ya hisia kisiasa Mlima Kenya.