Habari

NMG Uganda kurejelea shughuli baada kufungwa kwa mwezi mmoja

July 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

NATION Media Group (NMG) Uganda sasa inatarajiwa kurejelea shughuli zake kikamilifu mwezi mmoja baada ya kufungwa mnamo Juni 28.

Hii ni baada ya kusitisha shughuli zake kufuatia operesheni ya kijeshi iliyozima matangazo ya vituo vyake vya televisheni na redio pamoja na kuathiri uchapishaji wa magazeti.

Kurejelewa kwa shughuli hizo kunafuatia mazungumzo ya ngazi ya juu yaliyohusisha Rais Yoweri Museveni, mwanawe na Mkuu wa Majeshi, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, pamoja na Mmiliki wa hisa nyingi za NMG, mfanyabiashara wa Tanzania Rostam Azizi.

Kampuni ya Taifa Group ilinunua asilimia 54.08 za hisa za NMG mapema mwaka huu na ikawa mwanahisa mkuu wa kampuni hiyo kubwa zaidi ya habari Afrika Mashariki.

Mwenyekiti wa Bodi ya NMG, Joe Muganda, alisema huduma zitaanza kurejeshwa hatua kwa hatua kupitia televisheni, magazeti, redio na majukwaa ya kidijitali.

“Tunaporejea kuwahudumia wasomaji na watazamaji wetu, tutazidi kujikita katika kutoa uandishi wa habari wa kuaminika, wenye usawa na taaluma katika majukwaa yetu yote,” akasema Muganda kupitia taarifa iliyotolewa Jumanne.