Trump aokoa maelfu ya ajira Kenya kwa kuongeza muda wa Agoa
MAELFUya wafanyakazi katika sekta ya nguo nchini Kenya wamepata afueni mpya baada ya Rais wa Amerika Donald Trump kutia saini sheria ya kuongeza muda wa Mpango wa Fursa na Ukuaji wa Afrika (Agoa) kwa miaka miwili zaidi, hatua inayohakikisha bidhaa za Kenya zinaendelea kuingia katika soko la Amerika bila ushuru hadi Desemba 31, 2028.
Uamuzi huo unaokoa takriban ajira 6,600 zilizokuwa katika hatari kutokana na kutokuwa na uhakika kuhusu mustakabali wa mpango huo wa kibiashara. Vilevile, unapatia kampuni zinazouza bidhaa Amerika muda zaidi wa kupanga uzalishaji na kuendelea kuhifadhi wafanyakazi wao.
Hatua hiyo inatarajiwa kurejesha imani katika eneo la bidhaa za kuuza nje (EPZ), ambako wawekezaji wamekuwa wakiahirisha maamuzi ya kupanua viwanda na kuwekeza zaidi kutokana na wasiwasi kuhusu hatima ya Agoa.
Sekta ya nguo na mavazi nchini Kenya inasaidia ajira zaidi ya 66,000 moja kwa moja katika uzalishaji, usafirishaji, masoko na shughuli nyinginezo. Pia hunufaisha mamia ya maelfu ya watu kupitia ajira zisizo za moja kwa moja na mapato ya familia.
“Tulikuwa na wasiwasi na tulikuwa tunafikiria kuwaachisha kazi baadhi ya wafanyakazi wetu kama sheria hiyo isingetiwa saini kwa wakati. Hii ndyio nafuu mkubwa zaidi kwetu,” alisema John Mwangu, mfanyabiashara wa mavazi Mombasa anayeuza bidhaa Amerika.
Waziri wa Biashara Lee Kinyanjui alikaribisha uamuzi huo akisema umetoa uhakika unaohitajika kwa wauzaji wa bidhaa nje ya nchi na wafanyakazi wanaotegemea soko la Amerika.
“Uamuzi wa Rais Donald Trump wa kuongeza muda wa Agoa hadi Desemba 31, 2028 ni wa kupongezwa sana,” alisema Kinyanjui.
Katika mwaka wa kifedha uliopita, Kenya ilipoteza ajira 5,337 katika maeneo ya EPZ huku nafasi zaidi ya 5,000 za ajira zilizotarajiwa kupatikana kupitia upanuzi wa viwanda zikikwama kutokana na kucheleweshwa kwa maamuzi ya uwekezaji.
Agoa ilianzishwa mwaka 2000 ili kuruhusu nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara kuingiza maelfu ya bidhaa katika soko la Amerika bila ushuru. Mpango huo uliwahi kuongezewa muda mara kadhaa, ikiwemo mwaka 2015 ulipoongezwa kwa miaka 10.
Mpango huo uliisha muda wake Septemba 2025 baada ya Bunge la Amerika kukosa kuuongeza kwa wakati, lakini ulirejeshwa kwa muda mwezi Februari mwaka huu hadi Desemba 2026. Sheria mpya sasa imeongeza muda huo hadi mwisho wa mwaka 2028.