Habari

Ufichuzi mpya kuhusu msichana aliyeanguka ghorofa ya sita mtaani Kilimani

Na KAMORE MAINA April 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAELEZO ya kina yameibuka kuhusu mwanamke aliyeaga dunia Jumapili asubuhi baada ya kuanguka kutoka ghorofa ya sita eneo la Kilimani, Nairobi.

Uchunguzi wa polisi unaashiria kuwa mhasiriwa, mwanafunzi wa chuo kikuu, alikuwa pamoja na mwanamume (ambaye amezuiliwa na polisi kwa sasa) waliyekutana naye kwenye tovuti maarufu ya kuchumbiana.

Huo ulikuwa mkutano wao wa kwanza baada ya kukutana mtandaoni.

Consolata Githinji, 22, mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Murang’a, na mwanamume waliyependana haraka, walibadilishana nambari za simu baada ya kukutana mtandaoni.

Baadaye walitumiana jumbe za mapenzi karibu kila siku.

Jumamosi iliyopita, mkutano wao wa ana kwa ana waliosubiri kwa muda mrefu uliwadia na Consolata akasafiri kilomita 85 hadi Nairobi.

Kinyume cha waliomtangulia Consolata waliopata wapenzi mtandaoni, mkutano huo uliashiria nyakati za mwisho za maisha yake.

Chumba

Consolata alianguka kutoka ghorofa ya sita ya jengo na kuangukia roshani ya ghorofa ya tatu na kufa papo hapo. Chumba alimokuwamo ni cha kukodisha kwa muda mfupi.

Polisi wanaochunguza kisa hicho wanasema walipata chumba hicho kimevurugika kuashiria uwezekano wa jaribio la mauaji.

Hata hivyo, walinzi na wafanyakazi wameeleza polisi kuwa hawakusikia tafrani yoyote kutoka chumbani humo hadi mwili wa mwanamke huyo ulipopatikana ukiwa umelowa damu.

Maafisa wa Idara ya Uchunguzi kuhusu Uhalifu (DCI) walimfikisha mpenziwe Consolata katika Korti ya Kibera, wakiomba muda wa kumweka korokoroni kusuburi wakamilishe uchunguzi.

Uchunguzi huo ulio katika hatua za mapema unanuiwa kubaini ikiwa kifo cha Consolata kilikuwa ajali au mauaji.

Mwanamume waliyekuwa naye Jumamosi usiku, ni mwenye umri wa miaka 33 anayefanya kazi katika kampuni inayosambaza bidhaa za nywele za wanawake.

Mwanamme huyo aliwasilisha stakabadhi zake za kitambulisho alipokodisha chumba hicho na Consolata.

Makachero pia wanamhoji mhudumu wa jengo hilo ambapo tukio hilo lilifanyika.

Aidha, wafanyakazi wawili waliokuwa kwenye zamu mkasa huo ulipotokea watahojiwa vilevile, mkuu wa DCI Nairobi, Daniel Kandie alisema jana.

Mwili wa Consolata umehifadhiwa katika Chumba cha kuhifadhia maiti cha Nairobi.