Habari

Uhuni na vurugu zatawala kampeni licha ya onyo la IEBC

Na SAMWEL OWINO na VITALIS KIMUTAI July 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) imewaonya wawaniaji dhidi ya kufadhili au kupanga ghasia kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
IEBC imesema kuwa wawaniaji wanaoshiriki tabia hizo watapigwa faini na pia uchaguzi utafutiliwa mbali kwenye maeneo yenye ghasia.
Kwenye mahojiano na Taifa Leo Mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon alisema tume hiyo itahakikisha mwongozo wa uchaguzi unafuatwa kuhakikisha kuna uwazi na uwajibikaji.
 “Hatuwezi kumruhusu mtu mmoja kuvuruga uchaguzi ambao unafadhiliwa na walipaushuru ili awe mbunge. Kama tume, tuna mamlaka ya kumpiga marufuku, kumtoza faini au hata kumzima mwaniaji ambaye amevunja sheria kushiriki uchaguzi,” akasema Bw Ethekon.
 Alisema IEBC haitakuvumilia uhuni wa kisiasa na haitajali mrengo ambao mwanasiasa anaegemea. Alisisitiza IEBC itachukua hatua kali kwa kutegemea ushahidi ambao utawasilishwa.
“Kama tuna ushahidi kuwa kuna mtu anawatumia wahuni, kuwalipa au kuwafadhili, basi mtu huyo anahujumu uchaguzi wa amani na atatozwa faini au kuzuiwa kuwania,” akasema.
Bw Ethekon alisema pia IEBC haitakuwa na budi ila kufutilia mbali uchaguzi katika maeneo ambako kuna utovu wa usalama.
Mwenyekiti huyo aliwataka wapigakura pia wanakili visa vya ghasia na aina yoyote ya uvunjaji wa sheria kisha wawasilishe ushahidi huo kwa IEBC.
“Umma haufai kushutumu tume kuwa haina meno ya kungáta bali pia wanakili uhalifu na matukio mengine kisha wawasilishe malalamishi kwetu. Ni kwa kutegemea ushahidi huu ndipo tutachukua hatua,” akasema.
Alisisitiza kuwa kuandaliwa kwa uchaguzi huru kunahitaji ushirikiano kutoka kwa washikadau wote.
Kauli, Bw Ethekon imekuja wakati ambapo kumekuwa na ghasia za kisiasa ikiwemo ya jana jijini Kisumu na hivi majuzi dhidi ya msafara wa Linda Mwananchi katika Kaunti ya Kisii.
Jana ghasia ziliibuka jijini Kisumu wakati ambapo wahuni walijaribu kuwauzuia Gavana wa Siaya James Orengo na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kuhudhuria ibada katika Kanisa la St Stephen Cathdral.
Wahuni hao walizuia wanasiasa hao wawili kuondoka na kuwalazimu polisi kutumia vitoza machozi kuwatimua.
Ghasia hizo zilichipuka baada ya Bw Orengo kuwahutubia waumini. Ilibidi Mabw Orengo na Sifuna waondolewe kupitia mlango wa nyuma.
Jana ilikuwa mara ya kwanza ambapo Bw Sifuna alijitokeza hadharani baada ya kubanduliwa kama katibu mkuu wa ODM.
“Nawashukuru sana wale ambao wamesimama nami tangu wakati nikihudumu kama katibu mkuu wa ODM,” akasema Bw Sifuna.
Suala hilo pia linatarajiwa litachipuka sana wakati ambapo Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen atafika mbele ya Kamati ya Bunge baadaye mwezi huu.
Akizungumza katika kikao cha faragha na wabunge mnamo Februari, Bw Murkomen alidai kuwa baadhi ya wanasiasa wanayafadhili makundi ya wahalifu wakijiandaa kwa uchaguzi.
“Suala la magenge ya wahalifu limekuwa gumu kwa polisi kwa sababu wanaoyafadhili wameketi katika Bunge hili, wanashikilia nyadhifa za juu serikalini na wana ushawishi mkubwa ndani ya vyama vya kisiasa. Kila wanapokamatwa, viongozi wa kisiasa huwatisha maafisa wa polisi wanaoshughulikia kesi hizo,” akasema
Mbali na hayo, Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja naye ameonya kuwa wahuni wa kisiasa na magenge ya uhalifu watakabiliwa vikali kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Alisisitiza Huduma ya Kitaifa ya Polisi haitaruhusu ghasia kuvuruga kampeni wala kuhatarisha usalama wa wananchi.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa afisi za Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) za Kaunti-ndogo ya Sotik katika Kaunti ya Bomet, Bw Kanja alisema watu wanaojihusisha na uhuni wa kisiasa, uhalifu uliopangwa na makosa mengine watafuatiliwa na kufikishwa mahakamani kwa mujibu wa sheria.
“Ninatoa onyo kwa wahuni na magenge ya uhalifu kote nchini kwamba watashughulikiwa kwa mujibu wa sheria na hawatapata nafasi ya kuendelea na shughuli zao,” akasema Bw Kanja.
Aliongeza kuwa kila mtu atawajibika binafsi kwa uhalifu wake na kuwaonya wanaojihusisha na ghasia za kisiasa kwamba watakabiliwa kibinafsi na matokeo ya vitendo vyao.
Inspekta Jenerali huyo alisema maafisa polisi 10,000 walioajiriwa mwezi Machi mwaka jana kwa sasa wanapitia mafunzo katika Chuo cha Mafunzo ya Polisi cha Kiganjo na watapelekwa katika maeneo mbalimbali nchini mara tu watakapohitimu ili kuimarisha juhudi za kuzuia uhalifu.