Habari

Wanablogu Murang’a wawindwa kwa madai ya kuchapisha taarifa za kukosoa serikali

Na MWANGI MUIRURI June 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MVUTANO umezuka Kaunti ya Murang’a, kati ya idara za usalama na wanablogu wanaotuhumiwa kuvuka mipaka ya uhuru wa kujieleza.

Kamati ya Usalama na Ujasusi ya kaunti hiyo imethibitisha kuwa imeanza operesheni ya kuwasaka wanablogu wanaodaiwa kuchapisha taarifa “zisizo na msingi na zenye madhara” mtandaoni.

Kamanda wa Polisi wa Murang’a Cleti Kimaiyo, alisema baadhi yao tayari wameagizwa kufika mbele ya maafisa wa usalama kueleza na kuthibitisha madai yao, akionya kuwa watakaokaidi watasakwa.

“Tumeanza kuwaita baadhi yao ili wafafanue walichochapisha. Wakikataa tutawatafuta popote walipo,” alisema.

Hata hivyo, hatua hiyo tayari imezua mjadala mkali wa kisiasa na kisheria.

Seneta wa Murang’a Joe Nyutu ameikosoa vikali, akiitaja kama njama ya kunyamazisha wakosoaji wa serikali na kuikosoa kama hatua ya kidikteta dhidi ya wasiounga mkono utawala wa Rais William Ruto.

Nyutu alisema baadhi ya wanablogu wanaolengwa tayari wamemtafuta wakitaka ushauri wa kisheria.

“Nimewaambia kuwa iwapo kuna madai ya kuchafua jina, Sheria ndiyo inapaswa kutumika. Kinachofanyika sasa ni kutumia mfumo wa haki ya jinai kuzima maoni tofauti ya kisiasa,” alisema.

Wakili James Muna wa Mahakama Kuu amesema amepitia baadhi ya machapisho na kubaini mengi ni ya kisiasa kuliko ya jinai.

Kwa mujibu wake, yanahusu kaulimbiu ya “Wantam”, kuhamasisha vijana, madai ya ufisadi ndani ya polisi, uporaji wa ardhi na ukosoaji wa sekta ya pombe.

“Ningeshauri mwanablogu yeyote aliyeitwa kuthibitisha madai kupuuza wito huo. Kuchafua jina ni suala la kiraia na huanza kwa notisi ya kudai maelezo au kuomba radhi, si kuitwa na polisi,” alisema.

Miongoni mwa wanaokabiliwa na msukosuko huo ni Mixson Warui, mwenye umri wa miaka 28 na anayetaka kugombea wadhifa wa kisiasa katika Wadi ya Kamahuha.

Alisema aliagizwa na maafisa wa usalama kuripoti makao makuu ya kaunti kutokana na machapisho yake.

“Walinielekeza niende kutoa taarifa lakini nilikataa. Sioni sababu ya kugharamia safari yangu ili nikamatwe. Wakitaka kunikamata, waje nilipo,” alisema.

Warui pia alidai amekuwa akipokea simu za vitisho kutoka kwa mtu anayejitambulisha kuwa sehemu ya kikosi cha utekaji nyara, akimtaka ajiandae kwenda gerezani au hata mabaya zaidi.

Mbunge wa Kigumo Joseph Munyoro alisema hatua hiyo inaonyesha viwango tofauti vinavyotumika kushughulikia maoni ya kisiasa mtandaoni.

“Wanablogu wanaounga mkono serikali huwatusi viongozi wa upinzani kila siku bila kuchukuliwa hatua, lakini wakosoaji ndio wanaitwa na polisi,” alisema.

Kwa upande wake, Afisa Mkuu wa Vijana na Michezo wa Murang’a Manoah Gachucha alisema mazingira ya vitisho dhidi ya wanaharakati mtandaoni yamekuwepo kwa takriban miezi 19.

Alitaja kifo cha Dennis Mwangi, kijana mwenye umri wa miaka 28 aliyedaiwa kutekwa nyara kabla ya kupatikana amefariki Januari 2025, kama mfano wa hali hiyo.

Lakini maafisa wa usalama wanasisitiza kuwa operesheni hiyo inalenga kukomesha kusambaa kwa taarifa za uongo na zinazoweza kuhatarisha usalama wa umma.

Hata hivyo, mwanasheria wa haki za binadamu Timothy Kariuki ameonya kuwa baadhi ya vifungu vinavyotumiwa na maafisa wa usalama vilifutwa na Mahakama ya Rufaa mwaka 2023.

“Sheria iko wazi. Hauwezi kufanya kauli kuwa kosa la jinai kwa sababu tu serikali haifurahishwi nayo,” alisema.