• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 1:33 PM
AFYA: Hofu ya wanaume ‘mlingoti’ kukosa kusimama wima chumbani

AFYA: Hofu ya wanaume ‘mlingoti’ kukosa kusimama wima chumbani

NA BENSON MATHEKA

Idadi ya watu wanaoendelea kupoteza maelfu ya pesa wakitafuta suluhu ya kupungukiwa na nguvu za kiume ikiwa ni pamoja na kutafuta huduma za waganga inazidi kuongezeka.

Na ushauri wanaopata kutoka kwa matabibu bandia umewafanya wengi kujuta baada ya kulaghaiwa pesa na mali yao. Kote mitaani kuna wataalam bandia wanaodai kwamba wana uwezo wa kutibu maradhi sugu ya upungufu wa nguvu za kiume.

Wataalamu hao wa mitaani wamekuwa wakivuna donge nono hasa kutoka kwa wanaume wanaosumbuliwa na matatizo ya ukosefu wa nguvu za kiume. Hata hivyo, wataalamu wa afya wanasema tatizo la upungufu wa nguvu za kiume sio kurogwa.

Utafiti wa shirika la National Ambulatory Medical Care, NAMCS, umeanika wazi matatizo yanayosababisha upungufu wa nguvu za kiume na athari zake.

NAMCS ilifichua kuwa hali hii inachangia ongezeko la talaka na migogoro ya kinyumbani kwa sababu wanaume wengi wamekuwa hafifu kutekeleza tendo la ndoa.

Wanaume 75 kati ya 100

Kwa mujibu wa utafiti huo, kwa kila wanaume 100, 75 kati yao husumbuliwa na tatizo la upungufu wa nguvu za kiume hasa wale wenye umri wa kuanzia miaka 40 kuendelea. Aidha, kutokana na kukithiri kwa tatizo hilo, NAMCS inasema wanaume wengi wameanza kutumia dawa za kuongeza nguvu za kiume zinazowadhuru kiafya na kuonngeza matatizo yao.

“Asilimia 5 ya wanaume wenye umri wa miaka 40 na kuendelea wamekuwa wakihangaika kutafuta tiba. Na kati ya asilimia 15 na 25 ya wanaume wenye umri wa miaka 65 wanakabiliwa na tatizo hilo,” yaeleza ripoti hiyo.

Katika jamii ya Kiafrika kuna dhana potovu kuwa kupoteza nguvu za kiume hutokana na uchawi na ndio sababu ya wengi kugeukia waganga ambao wanatumia fursa hiyo kuwalaghai.

Kulingana na Dkt Ngaruiya Moses, ambaye ni mtaalamu wa afya ya uzazi katika hospitali ya Scion, Nairobi, hali hii inaweza kusababishwa na kuwepo kwa sehemu iliyo katika kiungo cha uzazi cha mwanaume iitwayo corpus cavernosum ambayo kwa sababu tofauti huugua na kumfanya mwanaume kupoteza nguvu.

Aidha, anasema kuwa tatizo la upungufu wa nguvu za kufanya mapenzi huanzia kwenye ubongo na hata kumfanya mwanaume kupoteza hamu ya kufanya mapenzi na wanaume hawafai kudaganywa na waganga.

Daktari huyo anaeleza kuwa maradhi ya moyo, figo na kifua yanaweza kumfanya mwanaume kushindwa kuwa imara kwa tendo la ndoa. Tatizo hili pia huwapata watu walio na shinikizo la damu ambao hukosa nguvu za kiume.

Utafiti wa NAMCS unafafanua kuwa wanaume wanaobugia pombe kwa wingi, wavutaji wa sigara, watafunaji wa miraa na walipooza mwili kutokana na maradhi, kunachangia katika hali hii.

“Maradhi sugu kama kisukari, zinaa na kuwa na mawazo kupita kiasi kunaweza kumfanya mwanaume kushindwa kutekeleza tendo la ndoa na sio uchawi kama waganga wanavyohadaa watu,” asema Dkt Ngaruiya.

Uzito kupita kiasi

Wengine walio katika hatari ya kupata tatizo hili, aeleza, ni wale wenye uzito kupita kiasi huku kati ya asilimia 10 na 20 wakisumbuliwa na tatizo hili kwa sababu ya athari za kisaikolojia.

Kinachotia wataalamu wa afya wasiwasi ni ukweli kwamba wengi wa waathiriwa hawaendi hospitali au kwa wataalamu waliohitimu kupata ushauri mbali, wanawatembelea waganga wanaowahandaa kuwa wana dawa za tatizo hili.

Utafiti wa NAMCS unafichua kuwa wanaume wengi huona haya kuelezea tatizo hili wasichekwe na kudharauliwa.

Kuchekwa na kudharauliwa

“Hata hivyo, ukweli ni kuwa, watu wengi husema uongo ili waonekane kuwa ni wanaume hasa mbele ya wenzao huku wangine wakigubikwa na nadharia duni,” yasema sehemu ya utafiti wa NAMCS.

Daktari Ngaruiya anataja lishe duni na matumizi ya mihadharati kama chanzo cha tatizo hili miongoni mwa vijana. Nao ‘waganga wa kienyeji’ wamegundua migodi ya pesa kutoka kwa walio na tatizo hili.

Wameweka mabango kujivumisha na hata kulipa matangazo kwenye vyombo vya habari wakijigamba kuwa wana dawa kali za kuongeza nguvu za kiume.

“Hii inadhihirisha hali halisi ilivyo. Ni watu wengi walionaswa na matangazo haya na sasa wanajuta baada ya kutumia pesa nyingi bila kupata afueni,” aeleza Michael Karanja, mwanasaikolojia katika kituo cha Maisha Mema jijini Nairobi.

Wataalamu wanahofia kuwa huenda waganga hawa wakawapatia wateja wao dawa hatari zinazoweza kuwadhuru na hata kuwaua.

“Wako katika biashara na wanaweza kuwapa wanaowatembelea dawa yenye sumu na kuwaangamiza,” asema Bw Karanja. Baadhi ya wanaume wanakiri kuwa waliwatembelea waganga hawa kupata tiba ya kupungukiwa na nguvu za kiume.

Kupungua kwa nguvu miongoni mwa wanaume wengi kumesababisha wengi wao waishi katika maisha na hali ya kusononeka na wengine wameripotiwa kujiua kutokana na hali hiyo.

Wataalamu wa afya wanaamini kuwa mara nyingi hali hiyo, hasa kwa watu wenye umri wa chini ya miaka 45, husababishwa na msongo katika akili hasa wasiofanya kazi nyingi.

“Watu wengi wanaofikiri kuwa wamepungukiwa na nguvu hizo huwa wako sawa,” yasema sehemu moja ya utafiti uliofanywa na wataalamu wa Chuo Kikuu cha Havard, nchini Amerika.

Utafiti huo unafafanua kuwa tatizo la watu hao huwa ni kushiriki tendo hilo kwa wakati usiofaa.

“Wanashiriki wakiwa hawajajitayarisha kiakili,” wasema wataalamu wa Havard. Wanaeleza kuwa tatizo hilo huwapata wanaume wengi kwa sababu ya utumiaji wa vyakula vinavyoongeza kiwango cha mafuta mwilini ambao hawashiriki katika mazoezi ya viungo.

Hii huifanya misuli ya damu mwilini kutofanya kazi vizuri na hivyo kusababisha matatizo mengi na mwili kushindwa kufanya kazi zake ipasavyo.

Tendo la ndoa

Idadi ya wanaume wanaokabiliwa na tatizo la kushindwa kutekeleza tendo la ndoa imeongezeka.

“Waganga wa kienyeji wamekuwa wakivumisha huduma zao kwa sababu wanajua kuna wateja hapa nchini. Kuna haja ya kampeni kufanywa ili kuwaeleza watu ukweli wa mambo na wanayopasa kufanya wakipatwa na matatizo kama haya,” akasema.

Anasema watu wengi wamegeukia matumizi ya tembe za kuongeza nguvu za kutekeleza tendo la ndoa kama vile Viagra bila ushauri wa daktari jambo ambalo limewasababishia matatizo zaidi ikiwa ni pamoja na kifo.

Kulingana na mtaalamu huyu, tembe hizi ni hatari na zinapaswa kutumiwa kwa ushauri wa daktari pekee.

“Watu hupata tatizo la kupungukiwa na nguvu za kiume kwa sababu tofauti na kwa hivyo ni daktari pekee anaweza kushauri mtu matibabu yanayofaa.

Inasikitisha kuona hata vijana wadogo wakitumia tembe za kuongeza nguvu za kutekeleza tendo la ndoa na kukatiza maisha yao,” aeleza.

You can share this post!

NGILA: Tulinde watoto dhidi ya dhuluma kwenye mitandao

AFYA: Usikimbilie vidonge madukani, nenda kwa daktari...

adminleo