Jamvi La Siasa

Kindiki anasukumwa kona mbaya Mlimani

Na BENSON MATHEKA June 1st, 2025 Kusoma ni dakika: 3

NAIBU Rais Kithure Kindiki anakumbwa na upinzani mkali katika ngome ya Mlima Kenya, huku wanasiasa waliokuwa washirika wa serikali wakihamia upande wa upinzani na kuapa kung’oa serikali ya Kenya Kwanza madarakani mwaka 2027.

Kinachomfanya Profesa Kindiki kuonekana kuwa pabaya uchaguzi mkuu unapokaribia ni kuungana kwa wanasiasa wakuu kutoka Mlima Kenya Mashariki, eneo linalochukuliwa kama ngome yake ya kisiasa.

Naibu Rais huyo wa tatu wa Kenya anatoka kaunti ya Tharaka Nithi ambayo pamoja na Meru na Embu zinaunda Mlima Kenya Mashariki.

Japo anasisitiza kuwa ni raia watakaofanya uamuzi wa mwisho debeni na kwamba kazi yake ni kusaidia Rais Ruto kutimiza ahadi za uchaguzi, waziri huyo wa zamani wa usalama wa ndani anaonekana kutumia nguvu za serikali huku akimwaga pesa kwa makundi ya wakazi kuwavutia waunge serikali.

Amekuwa akikutana na jumbe za viongozi wa mashinani kuuza ajenda za serikali, mbinu ambayo wachanganuzi wa siasa wanasema huenda isimsaidie iwapo vigogo wa kisiasa kutoka eneo hilo wataendelea kuungana kupiga vita serikali.

“Kila dalili zinaonyesha kuwa Profesa Kindiki anaendelea kubanwa na kwa kuzingatia jinsi vigogo wa upinzani kutoka inayochukuliwa kuwa ngome yake ya Mlima Kenya Mashariki wanaendelea kuungana, litakuwa pigo kubwa kwake,” asema mchanganuzi wa siasa James Kihara.

Katika mkutano wa hadhara wa viongozi wa upinzani uliofanyika mjini Matuu mnamo Ijumaa, Mei 30, aliyekuwa Waziri wa Kilimo Mithika Linturi anayetoka Meru alimshambulia vikali Profesa Kindiki kwa kile alichokitaja kama “ziara zisizo na maana” katika eneo la Meru na Mlima Kenya kwa ujumla.

“Kwa sasa, Ruto halali. Naibu wake anatembelea Meru angalau mara kumi kwa wiki moja,” alisema Linturi.

Aliongeza kuwa wakazi wa Meru na Mlima Kenya hawapo tena upande wa serikali, akisema kuwa wameamua kusonga mbele kutafuta mwelekeo mpya wa kisiasa.

“Tayari tuna kura za Mlima Kenya, Meru, Magharibi na Ukambani. Tunaanza na takribani kura milioni nane. Mpango huu umeiva,” alisema Linturi, ambaye ni afisa wa juu wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP) cha Rigathi Gachagua, mtangulizi wa Profesa Kindiki kama naibu rais.Kwa mujibu wa duru za kisiasa, hatua ya aliyekuwa Gavana wa Meru, Peter Munya, kujiunga na upinzani ni pigo kubwa kwa Kindiki.

Munya anajiunga na viongozi wengine waliowahi kuwa serikalini kama vile Justin Muturi ambao sasa wamejiunga na Rigathi Gachagua na wote wamekuwa wakishambulia serikali ya Ruto na mrithi wake, Kindiki.

Bw Kiarie anasema hii inadhihirishwa na hasira za wakazi kwa wasanii waliomtembelea katika makazi yake rasmi mtaani Karen, Nairobi.

Mashabiki walimiminika kwenye mitandao ya kijamii kuwalaumu vikali wasanii hao kwa kile walichokitaja kama ‘usaliti’ kwa jamii ya Wakikuyu, huku wengine wakitishia kususia muziki na maonyesho yao.

Viongozi wengine wa kisiasa waliokuwa kwenye kikao hicho Karen walijumuisha Mbunge wa Thika Alice Ng’ang’a, John Njuguna Wanjiku (Kiambaa), Mburu Kahangara (Lari), Elijah Njoroge (Gatundu Kaskazini), na Githua Wamacukuru (Kabete) ambao wachanganuzi wanasema hawana ushawishi kama vigogo wanaohamia upinzani.

Huku mvutano huu ukiendelea, wadadisi wanasema tukio hili limeweka wazi hali tete ya kisiasa kati ya viongozi wa Mlima Kenya wanaohusishwa na serikali na wale wanaojaribu kujiweka upande wa wananchi wakidai kubaguliwa na kusahaulika.

Bw Muturi, ambaye aliondolewa kazini kwa kuikosoa baada ya utekaji nyara wa vijana, amekuwa mkosoaji mkubwa wa serikali, akiishutumu kwa kushindwa kulinda haki za kibinadamu hasa vijana waliokuwa mstari wa mbele katika maandamano.

Kiarie anasema Kindiki aliteuliwa kurithi Gachagua ili kulinda kura za Mlima Kenya lakini anaonekana kukosa ushawishi mpana wa kurejesha eneo hilo kwa serikali ya Kenya Kwanza.

“Ni wazi kuwa hali ya kisiasa imebadilika Mlima Kenya na hali hii inamweka Kindiki katika kona mbaya kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Sidhani juhudi zake za kutumia jumbe na kumwaga pesa katika eneo hilo zitabadilisha hali ikizingatiwa vigogo wa kisiasa wanaonekana kuungana dhidi yake,” asema Kiarie.Hali ikisalia hivi, Kindiki atakuwa na wakati mgumu sana kuelekea katika uchaguzi mkuu wa 2027.