Mfumo wa baridi wafungua soko la kimataifa kwa wakulima wa maparachichi
KWA miaka mingi, wakulima wa maparachichi katika Kijiji cha Cura, Kiganjo, Kaunti ya Kiambu, walikuwa wakihangaika kupata faida kutokana na jasho lao.
Walikabiliwa na madalali waliowalipa bei duni, kuchelewesha malipo au hata kutowalipa kabisa, huku sehemu kubwa ya mazao yao ikiharibika kwa kukosa njia bora za kuhifadhi.
Leo hii, simulizi hiyo imebadilika. Kupitia teknolojia ya maghala ya baridi yanayotumia umeme na nishati ya jua, wakulima hawa sasa wanapata bei nzuri, malipo ya haraka na fursa za kuuza maparachichi yao katika masoko ya kimataifa.
Miongoni mwa walionufaika ni John Mburu Ndotono, ambaye alianza kulima maparachichi mwaka 2016 baada ya kuachana na ufugaji wa ng’ombe wa maziwa. Anakumbuka jinsi madalali walivyokuwa wakitumia udhaifu wa wakulima kujinufaisha.
“Walikuwa wakinunua kilo moja kwa kati ya Sh3 na Sh5. Wakati mmoja walivuna kilo 1,500 katika shamba langu na kuahidi kurudi kuchukua zilizobaki, lakini hawakurudi kamwe. Matunda yaliishia kuozea shambani,” anasimulia.
Lucy Mumbi naye anakumbuka kuuza kila tunda kwa Sh2.50 pekee. Mara kadhaa mabroka walipakia mazao kwenye lori na kutoweka bila kufanya malipo. “Mkulima alikuwa hana sauti wala uwezo wa kujitetea,” anasema.
Changamoto hizo zilichangiwa zaidi na ukosefu wa miundombinu ya kuhifadhi mazao baada ya mavuno. Kwa kuwa maparachichi huharibika haraka, wakulima walilazimika kuuza mara moja baada ya kuvuna, hata kwa bei ya hasara.
Misimu ya mavuno mengi, hadi nusu ya mazao yalipotea. James Mwangi Kibunjaanasema baadhi ya madalali walikuwa wakitumia ujanja hata wakati wa kuvuna. “Ungeambiwa wamechukua matunda matano, lakini kwa siri wanaongeza mengine mawili au zaidi. Mkulima ndiye alikuwa akipoteza kila mara,” anasema.

Hali hiyo imeanza kubadilika kupitia kampuni ya Soko Fresh, ambayo imeanzisha vituo vya kuhifadhi maparachichi katika mazingira ya baridi na kuunganisha wakulima wa mashamba madogo na wanunuzi wa nje ya nchi.
Kulingana na Stephen Katingima, Afisa Mkuu wa Mikakati wa kampuni hiyo, zaidi ya asilimia 80 ya maparachichi nchini huzalishwa na wakulima wadogo, lakini kwa muda mrefu walikosa nafasi katika biashara ya kuuza nje.
“Lengo letu ni kuhakikisha wakulima hawa wanashiriki kikamilifu katika masoko yenye thamani kubwa na kunufaika na bei bora,” anasema.
Soko Fresh sasa inashirikiana na zaidi ya wakulima 15,000 na imeanzisha vituo zaidi ya 32 vya kuhifadhi mazao kwa mfumo wa baridi. Teknolojia hiyo imepunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno na kuboresha ubora wa matunda yanayopelekwa sokoni.
Matokeo yake yameashiria kuzaa matunda kwa wakulima. Mburu sasa huuza maparachichi yake kwa kati ya Sh80 na Sh100 kwa kilo, ikilinganishwa na Sh3 hadi Sh5 aliyokuwa akipata hapo awali. “Sasa nina soko la uhakika na malipo yanayofanyika kwa wakati. Maisha yangu yamebadilika kabisa,” anasema.
Alice Wangari anasema malipo hufanyika ndani ya dakika 30 baada ya kuwasilisha mazao. Kwa upande wake, Doreen Khaule, ambaye ana zaidi ya miti 200 ya maparachichi katika ekari moja, sasa hupata karibu Sh90 kwa kilo badala ya Sh6 hadi Sh10 alizokuwa akilipwa miaka ya nyuma. “Maparachichi sasa yamekuwa chanzo kikubwa cha kipato. Ninaweza kulipa karo ya watoto na kulea familia yangu kwa urahisi,” anasema.

Kulingana na Katingima, mwaka uliopita Soko Fresh ilisafirisha tani 300 za maparachichi katika masoko ya kimataifa huku ikihudumia karibu wakulima 5,000. Matunda ya ubora wa juu huuzwa kwa kati ya Dola 1.9 na 2.1 za Amerika kwa kilo, huku wakulima wakipata hadi Sh120 kwa kilo kulingana na kiwango cha ubora.
Ukuaji huo umeungwa mkono na ufadhili kutoka Global Energy Alliance for People and Planet (GEAPP) kwa ushirikiano na CLASP. Kati ya mwaka 2021 na 2024, mashirika hayo yaliwekeza Dola milioni 6.1, sawa na takriban Sh788 milioni, kusaidia kampuni zinazotumia teknolojia kuboresha kilimo katika nchi sita za Afrika, ikiwemo Kenya.
“Tunasaidia kupunguza hatari za uwekezaji ili kampuni ziweze kupanua huduma zao na kufikia wakulima wengi zaidi,” anasema Carol Koech, Makamu wa Rais wa GEAPP Afrika.
Licha ya mafanikio hayo, wakulima bado wanakabiliwa na changamoto kadhaa, zikiwemo gharama kubwa za pembejeo, wadudu na magonjwa, wizi wa mazao, gharama za kupata vibali vya viwango vya kimataifa na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Hata hivyo, kutokana na kuimarika kwa mifumo ya kuhifadhi mazao na kuongezeka kwa upatikanaji wa masoko ya nje, wakulima wengi wa maparachichi wanaona siku za kuuza mazao yao kwa bei ya kutupa zikibaki kuwa historia. Mfumo wa baridi sasa umegeuka kuwa daraja linalowaunganisha na masoko yenye faida kubwa duniani.