Habari Mseto

Mama aua wanawe 2 Bomet, kisha kujinyonga kwa kamba

Na VITALIS KIMUTAI August 5th, 2024 1 min read

MAJONZI yamegubika familia moja katika kijiji cha Chebisian, Kaunti ya Bomet baada ya mama aliyedaiwa kusongwa na mawazo kuua wanawe wawili kabla ya kujitoa uhai.

Ilidaiwa kuwa Bi Cherono, 35, aliangamiza watoto wake, Abigael Chepkorir, 10, na Amos Kipchirchir, 5, kwa kutumia silaha butu kabla ya kujinyonga Jumamosi, Agosti 3, 2024.
Mtoto wa Cherono aliyesalia ni mvulana ambaye ni mwanafunzi wa shule ya upili aliyekuwa kaunti ya Kericho wakati wa tukio.
Mama huyo na wanawe walikuwa pekee yao katika nyumba ya kakake, mkasa huo ulipotokea, kwani watu wengine wa familia hiyo hawakuwepo.
“Nilikuwa mjini Kericho na mke wangu alikuwa amewatembelea wakwe zangu, na dadangu akasalia nyumbani. Hakuonyesha dalili zozote za msongo wa kiakili kwani niliwasiliana naye kwa njia ya simu Ijumaa (Agosti 2, 2024), siku moja kabla ya kisa hicho kutokea,” akasema David Bett, ambaye ni kakake Cherono.

Bw Bett alisema aliporejea Jumamosi alifululiza katika Kanisa la Kiadventista la Merigi akitarajia kukutana na familia yake huko.
“Ibada ilipokuwa ikiendelea, niliitwa na binamu yangu aliyenijuza kuhusu kilichotokea. Niliingia kwenye gari lake na tukaelekea nyumbani. Tuliwapata wanakijiji wakiwa wamejazana nyumbani,” Bett akaambia Taifa Dijitali.