Michezo

Korir azoa Sh25m Lokedi akivuna Sh19m Boston Marathon

Na MWANDISHI WETU April 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KENYA ilisherehekea ushindi wa kihistoria katika mbio za Boston Marathon 2026 Jumatatu baada ya John Korir na Sharon Lokedi kutetea mataji yao kwa kishindo wakivuna Sh25,830,000 (USD200,000) na Sh19,372,500 (USD150,000), mtawalia.

Korir alionyesha ustadi wa aina yake akitwaa taji la wanaume kwa rekodi mpya ya Boston Marathon na pia muda wake bora mpya wa saa 2:01:52.

Alikuwa katika kundi kubwa lililokuwa likiongoza kabla ya kuongeza kasi kwa nguvu katika eneo la Heartbreak Hill, akimpita Muethiopia Milkesa Mengesha na kufungua mwanya mkubwa uongozini.

Muda wake uliivunja rekodi ya awali ya Boston Marathon iliyowekwa na Geoffrey Mutai mwaka 2011 ya 2:03:02, na pia kuboresha rekodi yake binafsi ya awali ya 2:02:24.

Korir sasa ni mtimkaji mwenye kasi bora wa mbio hizo za kilomita 42 duniani mwaka huu.

Mtanzania Alphonce Simbu alimaliza wa pili kwa 2:02:47, huku Benson Kipruto akifunga tatu-bora kwa 2:02:50.

Katika mbio za wanawake, Lokedi alitetea umalkia wake kwa 2:18:51. Alikuwa ndani ya kundi lililoongoza lililojumuisha Irine Cheptai, Loice Chemnung na Mary Ngugi-Cooper kabla ya kuongeza kasi katika vilima vya Newton na kujitenga mwishoni.

Chemnung alikamata nafasi ya pili kwa 2:19:35, Ngugi-Cooper akawa wa tatu kwa 2:20:07, huku Mercy Chelangat akikamilisha ushindi wa kihistoria wa Kenya kwa nafasi nne za kwanza.

Rais William Ruto pamoja na Waziri wa Michezo Salim Mvurya waliongoza Wakenya kusherehekea mafanikio hayo ya kihistoria.

Boston Marathon ni ya pili katika ligi ya Marathon Kuu Duniani (WMM) mwaka huu baada ya Tokyo Marathon mwezi uliopita.

Ni mara ya kwanza tangu mwaka 1996 kwa mabingwa wa Boston Marathon kuhifadhi mataji yao.

Licha ya muda hiyo bora, barabara za mbio za Boston Marathon haziruhusiwi kutambuliwa kama rekodi rasmi za dunia.