Sports Kenya: Waandamanaji walipora na kuharibu Nyayo
WAKATI ambapo Kenya inajizatiti kukamilisha miundomsingi yake kabla ya kipute cha Kombe la Afrika kwa wachezaji wanaoshiriki ligi za nyumbani (CHAN), bidii hiyo imerejeshwa nyuma baada ya uga wa Nyayo kuharibiwa.
Maandamano ya Jumatano hayakusaza uwanja huo huku Shirika linalosimamia viwanja nchini, Sport Kenya likithibitisha waandamanaji waliharibu vifaa ugani Nyayo.
“Ni ukweli uga wa Nyayo uliharibiwa vibaya wakati wa maandamano ya Jumatatu. Kwa sasa tunaendelea kutathmini na kukadiria hasara kabla hatujatoa ripoti kamili,” akasema afisa wa mawasiliano wa Sport Kenya Rakki Asman.
Maandamano yalikuwa yakiendelezwa na vijana nchini kuadhimisha mwaka moja tangu mauti ya Gen Z. Hata hivyo, yaliishia fujo maeneo mbalimbali nchini huku Shirika la Kimataifa la Amnesty likisema watu 16 waliuawa nao zaidi ya 500 wakipata majeraha mbalimbali, baadhi yakiwa ya risasi.
“Vioo katika sehemu ya ndani ya uwanja viliharibiwa na vifaa vingi kuibwa. Jengo la Swimming Complex ambalo pia lina hoteli ndani pia liliharibiwa na bidhaa nyingi kuibwa,” akaongeza Asman.
Pia duru ziliarifu waandamanaji hao waliingia hadi vyumba vya wachezaji kubadilishana nguo na kutekeleza uharibifu mkubwa.
Uharibifu huo unakuja wakati ambapo Kenya imekuwa ikipambana kuhakikisha kuwa nyuga zake zinakuwa tayari kwa Chan ambayo itaanza Agosti 2 na kuisha Agosti 30.
Kenya pamoja na majirani zake Uganda na Tanzania zitaandaa Chan na zilikuwa na makataa ya Juni 25 (Jumatano) kukabidhi nyuga zake zote kwa Shirikisho la Soka Afrika (CAF).
Nyayo ni kati ya nyuga ambazo zinastahili kutumika pamoja na Kasarani kuandaa mechi za CHAN.
Ulinzi Sports Complex, Police Sacco, Kirigiti, Kasarani Annex “A” na “B” na nyuga mbili katika Akademia ya Michezo (KAS) iliyoko Kasarani nazo ziliorodheshwa kutumika kwenye mazoezi ya mashindano hayo ya Afrika.
Mnamo Ijumaa wiki jana, maandalizi duni na ukarabati wa kujikokota wa nyuga ulisababisha CAF ipokonye Kenya hati ya kuwa mwenyeji wa mechi za Kundi D.
Mitanange hiyo sasa itachezwa Zanzibar na itashirikisha mechi za mibabe na timu za nguvu kama mabingwa watetezi Senegal, Congo, Sudan na Nigeria.
Kenya itaandaa fainali ya CHAN na mechi za Kundi A ambazo ni Kenya, Morocco, Angola, DR Congo na Zambia.