Kimataifa

Mkewe rais wa zamani wa Zambia, Maureen Mwanawasa aaga dunia


LUSAKA, Zambia

ALIYEKUWA Mama wa Taifa nchini Zambia Maureen Mwanawasa amekufa akiwa na umri wa miaka 61.

Aliaga dunia Jumanne, Agosti 13, 2024, jioni akipokea matibabu katika hospitali moja jijini Lusaka baada ya kuugua kwa muda mfupi, familia yake ilisema.

Bi Mwanawasa ni mkewe Rais wa tatu wa Zambia Levy Mwanawasa, aliyeongoza taifa hilo kuanzia mwaka wa 2002 hadi alipoaga dunia mnamo mwaka wa 2008.

Rais Hakainde Hichilema alituma risala za rambirambi akielezea kupokea habari za kifo cha Bi Mwanawasa “kwa mshtuko mkubwa.”

Kabla ya kifo cha mumewe mnamo 2008, Bi Mwanawasa alipigiwa upatu kurithi urais lakini baadaye aliamua kutowania wadhifa huo.

Mnamo mwaka wa 2016, mwendazake aliwania kiti cha Meya wa jiji la Lusaka lakini akabwagwa.