Habari za Kitaifa

Mugaa, waziri mteule ‘maskini’ ambaye utajiri wake ni Sh31 milioni tu

Na CHARLES WASONGA August 2nd, 2024 1 min read

WAZIRI mteule wa Maji, Usafi na Unyunyiziaji Eric Muriithi Mugaa amefichua kuwa thamani ya mali yake ni Sh31 milioni japo hamiliki gari.

Mhandisi Mugaa Ijumaa alielezea wanachama wa Kamati ya Bunge kuhusu Uteuzi kuwa, mali yake inatokana na kilimo cha majani chai, kahawa, ndizi na miraa, eneo bunge la Igembe Kusini, Kaunti ya Meru alikozaliwa.

Mwenyekiti wa kamati hiyo Spika Moses Wetang’ula alipotaka kufahamu sababu ya yeye kutomiliki gari ilhali thamani ya mali yake ni Sh31 milioni, Mugaa alijibu hivi: “Niliamua kuwekeza katika kilimo badala ya gari.”

Kufikia sasa, Waziri mteule huyo ndiye mwenye kiwango cha chini zaidi cha utajiri miongoni mwa wanane ambao wamepigwa msasa na kamati hiyo kufikia sasa.

Mugaa, 32, ndiye waziri mteule mwenye umri mdogo zaidi miongoni mwa wenzake watu 21 waliopendekezwa na Rais William Ruto kushikilia nyadhifa mbalimbali.