Habari Mseto

Raila Odinga aungana na watoto yatima kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa

January 7th, 2024 1 min read

NA ALEX KALAMA

KIONGOZI wa upinzani Raila Odinga Jumapili, Januari 7, 2024 aliungana na kituo cha watoto yatima cha Malindi Orphanage, ili kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa.

Kinara huyo wa muungano wa Azimio la Umoja alizaliwa mnamo Januari 7, 1945 na ameadhimisha miaka 79 ya kuzaliwa.

Kwenye ziara yake katika kituo hicho chenye makao yake katika wadi ya Shella, Malindi, Kaunti ya Kilifi alitoa msaada wa bidhaa mbalimbali, ikiwemo chakula.

Bw Odinga alikuwa ameandamana na mkewe Mama Ida Odinga, viongozi kadha wa chama cha ODM, akiwemo Gavana wa Mombasa, Abdulswamad Sharrif Nassir, Seneta wa Kilifi Steward Madzayo, wabunge; Ken Chonga wa Kilifi Kusini Ken Chonga na Amina Laura Mnyazi (Malindi).

Wengine ni Spika wa Bunge la Kilifi Teddy Mwambire, kiongozi wa wengi katika bunge la Kilifi, Ibrahim Matumbo, Naibu Gavana wa Kilifi, Florence Chibule na madiwani wa wadi mbalimbali Kilifi.

Bw Odinga pia ndiye kiongozi wa chama cha ODM.