Hatutachezea uteuzi chamani ODM tena, Oburu ahakikishia wafuasi
KIONGOZI wa ODM, Dkt Oburu Oginga ametangaza kuwa mara hii chama hicho kitaandaa uteuzi wa haki na huru wala hakuna atakayependelewa kutokana na ukuruba wake na uongozi wa chama.
Dkt Oginga aliwaambia vijana wajitokeze kuwania viti kupitia ODM, akisema chama hicho kina mikakati ya kuanza kuchangamkia viongozi vijana mwaka wa 2027.
“Chini ya uongozi wangu nitahakikisha kuwa uteuzi ni huru na haki na vijana watakuwa na nafasi yao,” akasema Dkt Oginga, 82.
Alikuwa akiongea jana wakati wa Kongamano la Vijana wa ODM katika uwanja wa Jamuhuri Nairobi.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na vigogo wa ODM akiwemo Mwenyekiti Gladys Wanga na Waziri wa Madini Hassan Joho.
Kauli ya Dkt Oginga inakuja huku chama hicho kikipoteza viti kwa wapinzani miaka ya nyuma kutokana na mapendeleo kwenye uteuzi au kutoa tikiti za moja kwa moja.
Kwenye uchaguzi mkuu wa 2022, chama hicho kiliachia Jubilee kiti cha ugavana Nairobi licha ya kuwa mgombeaji wao Tim Wanyonyi (Mbunge wa Westlands) alikuwa na umaarufu na ugavana ukaishia kunyakuliwa na UDA.
Jana, Dkt Oginga aliweka bayana kuwa hawataingia mkataba wowote wa kuachiana viti Nairobi, akisema kuwa ODM inalenga kudumisha na hata kuongeza idadi ya viti vya ubunge.
“Tunalenga viti vingi zaidi ila lazima tuhakikishe watu wetu wanajisajili ndipo tuwe na kura nyingi,” akasema mbunge huyo wa Bondo. ODM imekuwa ikikabiliwa na maasi ya ndani ambapo kumeibuka makundi ya Linda Mwananchi na Linda Ground anayoingoza Dkt Oginga.
Jana alionekana akimlenga Katibu Mkuu Edwin Sifuna, akidai kuwa hawezi kuruhusu chama kugawanywa na viongozi wanaoenda kinyume na kinachokubaliwa kwenye mikutano ya viongozi wa ODM kisha kudai ni haki yao.
“Chama hakiwezi kuwa na fujo kupitia viongozi wanaosema mambo yao ya kibinafsi hapo nje kisha kudai ni ya chama. Mtu mmoja hawezi kuchukua msimamo na kuzungumza jambo tofauti kisha adai ni msimamo wa chama,” akaongeza.
Kauli yake iliungwa mkono na Gavana Wanga ambaye alisema ODM bado ni chama imara hata baada ya mauti ya Kinara wake Raila Odinga.
Mwenyekiti wa chama Kaunti ya Nairobi George Aladwa alisema mifumo ya chama lazima ifuatwe kuhakikisha kuwa wanadumisha umaarufu wao Nairobi.
“Tutamtetea kiongozi wetu wa chama na mnamo 2027 viti vyote vya ubunge Nairobi lazima ODM ivishinde. Binafsi nitakuwa nawania ugavana,” akasema Bw Aladwa.
Kila kiongozi aliyehutubu kwenye hafla hiyo alisema kuwa ODM lazima iwe makini kwenye muungano wake na UDA ili chama kisimezwe.