Abu Joho azuru maskani Pwani kunyanyua vijana wa mtaa akiendelea kujitambulisha kisiasa
BWANYENYE wa Mombasa, Abu Joho, ambaye pia ni ndugu wa Waziri wa Madini na Uchumi wa Bahari, Hassan Joho, amewahimiza vijana wa Pwani kutokata tamaa maishani na badala yake wajitume katika masomo na kutafuta fursa bora za maisha.
Akizungumza katika eneo la Changamwe, Bw Abu aliwataka vijana kuzingatia elimu hadi vyuo vikuu na vya kiufundi badala ya kukaa kwenye maskani bila mwelekeo.
Alitoa mfano wa nduguye Bw Joho, ambaye alisema alipata alama ya D- lakini baadaye aliendelea na masomo hadi kufika chuo kikuu na kufanikiwa hata kuwa Gavana wa kwanza wa kaunti ya Mombasa, na sasa ni Waziri katika serikali ya Kenya Kwanza.
“Nani ana B na hajaenda chuo kikuu? Msikate tamaa. Angalieni Hassan Joho alipata D- lakini aliendelea hadi chuo kikuu hata kile cha Harvard. Mungu, nidhamu na bidii ndio msingi wa mafanikio,” alisema.
Bw Abu alisema ataendelea kuzuru maskani mbalimbali katika kaunti ya Mombasa ili kuwatafuta vijana wasio na uwezo na kuwasaidia kupata ajira au kujiunga na vyuo vikuu.
“Ninawaahidi kuwa nitakuwa nikizuru maskani kuchagua vijana mwenyewe ili niwasaidie kupata ajira au wale wanaotaka kuendelea na masomo niwalipie karo. Nataka kusaidia yule asiye na mbele wala nyuma, yule ambaye amekata tamaa na hana wa kumtegemea isipokuwa Mungu,” alisema.
Aliongeza kuwa tayari ameajiri vijana wengi kutoka maskani na ataendeleza mpango huo. Katika eneo la Changamwe, alisema alichukua stakabadhi za vijana wenye shahada na kuahidi kuwasaidia kupata ajira.
Mwaka jana alisaidia zaidi ya vijana 10 kutoka mtaa wa Maweni kujiunga na vikosi vya polisi kupitia juhudi zake.
Hata hivyo, aliwaonya vijana dhidi ya kutumiwa na wanasiasa kuzua vurugu katika mikutano kwa ajili ya fedha.
Kwa wale ambao hawakufika kidato cha nne, Bw Joho alisema atawasaidia kupata vibarua ili waweze kujitegemea.
Alibainisha kuwa ameunda kikundi maalum cha kusaidia vijana wa Mombasa kupata ajira au kujiendeleza masomo.
Alisema kupitia juhudi hiyo ameweza kufanikiwa kuwabadilisha baadhi ya vijana waliokuwa wakijihusisha na uhalifu.
“Kuna waliokuwa wakibeba mapanga lakini sasa wameacha uhalifu na wanafanya kazi halali kwa sababu tuliwasaidia,” alisema.
Vile vile, aliwasihi vijana kujiandikisha kuwa wapigakura ili kushiriki kikamilifu katika kuchagua viongozi.