Siasa

Ruto avutia Mlima kwa ahadi ya ‘yangu 10, na ya Kindiki 10’ uchaguzi wa 2032

Na MWANGI MUIRURI April 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto sasa amekumbatia mbinu mpya ya kusaka uungwaji mkono katika eneo la Mlima Kenya akisema kuwa ‘atarudisha mkono’ mwaka wa 2032 kwa kuunga naibu wake Prof Kithure Kindiki.

Haya yanatokea baada ya Rais kupoteza ufuasi katika eneo hilo ambako alijizolea asilimia 87 ya kura mnamo 2022.

Kiini cha masaibu yake ni kutimuliwa kwa aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua mnamo Oktoba 2024.

Baada ya kutimuliwa, Bw Gachagua ameendelea kuwa mwiba kwa Rais Ruto baada ya kuanzisha chama cha DCP na kuongoza maasi dhidi ya Kiongozi wa Nchi eneo la Mlima Kenya.

Bw Gachagua, baada ya kutimuliwa, amejenga himaya yake ya kisiasa eneo hilo na kumchora Rais Ruto kama adui wa jamii ya Mlimani.

Juhudi ambazo Rais amekuwa akifanya kudumisha umaarufu wake eneo hilo hazijaonekana kuzaa matunda huku wandani wake wakizidi kuibuka na mikakati zaidi ya kuokoa hali.

Ni changamoto hizi ambazo sasa zimemfanya Naibu wa Rais aanze kusawiriwa kama mrithi wa Rais Ruto katika uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2032.

Rais, Prof Kindiki na baadhi ya wandani wao wamekuwa wakiashiria kuwa Prof Kindiki anaandaliwa kuwahi urais 2032.

Akiwa katika ziara ya Kaunti ya Kisii, Rais Ruto alisema Bw Gachagua hana subira, jambo lililomchongea.

“Ikiwa huna subira ya kuongozwa, hufai kuongoza,” akasema, kauli ambayo, ikitathminiwa sambamba na sifa ambazo amekuwa akimiminia Prof Kindiki, inaweka bayana siasa za urithi wa 2032.

Jumatatu, Mbunge wa Kapseret, Oscar Sudi, mwandani wa Rais, alisema njia pekee ya Mlima Kenya kurejea Ikulu ni kupitia ushirikiano wa kisiasa kati ya Rais Ruto na Prof Kindiki.

“Rais hafichi kuwa yeye ni zao la Mlima Kenya na angependa kushirikiana na eneo hilo sasa na siku zijazo katika kuunganisha nchi. Manaibu wanaoonyesha subira, uaminifu na bidii hufanikiwa, na Prof Kindiki ni mmoja wao,” akasema Bw Sudi.

Kwa upande wake, Prof Kindiki amedokeza wazi kuwa uaminifu wake kwa Rais Ruto ni mkakati wa kisiasa ikizingatiwa kuwa yuko karibu na kiti cha urais.

“Wakati mwingine si suala la mapenzi au kushabikia kiongozi ila ni kile ambacho unakilenga.”

“Rais Ruto ni kama ng’ombe wa maziwa mwenye mimba anayekaribia kuzaa na mimba hiyo ni mimi,” akasema Prof Kindiki.

“Nikisalia karibu na Rais, kupanda kwangu kisiasa kutachukua miaka mitano. Ikiwa mtu mwingine atachukua nafasi hiyo 2027, tutasubiri muda mrefu zaidi,” akaongeza.

Wandani wa Bw Gachagua, hata hivyo wamekosoa kauli hiyo wakisema Prof Kindiki analenga kutumia siasa za urithi kuvuruga miungano mipya ya kisiasa nje ya kambi ya Rais.

Kwa mujibu wa mchanganuzi wa masuala ya kisiasa, Dkt John Okumu, mvutano kati ya Prof Kindiki na Bw Gachagua unaanika wazi jinsi ambavyo siasa za urithi za 2032 zimeanza kushika kasi hata kabla ya kura ya 2027.

“Ni wazi kuwa Prof Kindiki na Bw Gachagua wanatofautiana kutokana na hesabu za uchaguzi wa 2027.”

“Faida ya mmoja ni hasara kwa mwingine ndiyo maana kuna mvutano mkubwa kati yao,” akasema Dkt Okumu.

Dkt Okumu anaona nafasi ya Prof Kindiki ikifanana na mikakati ya awali ya urithi wa uongozi, akirejelea makubaliano ya mnamo 2013 kati ya aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta na mgombeamwenza wake wakati huo, William Ruto (sasa rais).

Mchanganuzi mwingine Dkt Malila Munywoki naye anasema ni vigumu kwa Rais Ruto kutangaza wazi mpango wa urithi unaomhusisha Prof Kindiki kwa sasa.

“Itakuwa vigumu kwa Rais kusema wazi ‘kumi yangu, kumi ya Kindiki’ kwani hilo linaweza kutenga maeneo mengine na miungano ya kisiasa,” akasema Bw Munywoki.