Siasa

Uamuzi dhidi ya Gachagua sasa kero kwa Kindiki

Na MWANGI MUIRURI June 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UAMUZI wa Mahakama Kuu uliotolewa Jumatatu iliyopita wa kuthibitisha kuondolewa mamlakani kwa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua Oktoba 2024, umeibua changamoto mpya ya kisiasa kwa Naibu Rais Kithure Kindiki, hasa katika vita vya ushawishi kuhusu mwelekeo wa kisiasa wa eneo la Mlima Kenya kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Huku wandani wa serikali wakitarajia uamuzi huo ungepunguza ushawishi wa Bw Gachagua katika eneo hilo na kusababisha mabadiliko ya uungwaji mkono kuelekea kwa Profesa Kindiki, wengine wanasema hali imeonekana kuwa tofauti.

Rais William Ruto bado ana azma ya kurejesha ngome ya kura ya Mlima Kenya iliyomuunga mkono pakubwa katika uchaguzi wa 2022.

Hata hivyo, wachambuzi wanasema moja ya changamoto zake kubwa ni jinsi ya kupunguza ushawishi wa Bw Gachagua unaoonekana kuendelea kushamiri katika eneo hilo.

“Bila shaka Rais Ruto angependa kurejesha Mlima Kenya ambao kwa kiasi kikubwa ulimwezesha kuwa rais mwaka 2022. Changamoto yake ni jinsi ya kukabiliana na ushawishi wa Bw Gachagua. Baada ya kujaribu mbinu kadhaa za kisiasa katika kipindi cha miezi 20 iliyopita bila mafanikio makubwa, uamuzi wa kumwondoa ungekuwa na manufaa kwake iwapo wafuasi wa Gachagua wangeukubali kama kushindwa. Lakini hilo halijafanyika,” alisema Gavana wa Trans Nzoia, George Natembeya.

Bw Natembeya aliongeza kuwa uamuzi huo umeonekana kuibua huruma kwa Bw Gachagua hata nje ya nyanja za siasa, ikiwa ni pamoja na katika sekta ya sheria.

“Kilichojitokeza ni mjadala wa kitaifa, hata miongoni mwa wanasheria, wengi wao wakionyesha wasiwasi kuhusu hukumu iliyotambua ukiukaji wa haki za Gachagua lakini bado ikaidhinisha kuondolewa kwake,” alisema.

Seneta wa Murang’a, Joe Nyutu, alisema kulikuwa na matarajio kuwa Profesa Kindiki angepata nguvu zaidi kisiasa endapo wapigakura wa Mlima Kenya wangekubali uamuzi huo na kuendelea mbele bila Bw Gachagua.

“Hali sivyo ilivyo. Tunachoshuhudia ni maoni ya umma yanayoonekana kutoridhishwa na uamuzi huo, jambo linaloongeza upinzani dhidi ya serikali na kudhoofisha nafasi yake 2027,” alisema Bw Nyutu.

Kwa mujibu wa seneta huyo, Profesa Kindiki anahusishwa na matukio yaliyopelekea kuondolewa kwa Bw Gachagua madarakani.

“Katika fikra za wengi, Profesa Kindiki anaonekana kama aliyenufaika na mchakato wanaohisi haukuwa wa haki. Taswira hiyo imekuwa vigumu kuondoa,” alisema.

Hata hivyo, Mbunge wa Laikipia Mashariki Mwangi Kiunjuri alimtetea Naibu Rais, akisema ameingizwa bila haki katika mvutano wa kisiasa uliokuwepo kabla ya uteuzi wake.

“Profesa Kindiki alihudumu kama Waziri wa Usalama wa Ndani katika serikali ile ile ambayo Gachagua alikuwa Naibu Rais. Gachagua alitofautiana na viongozi wengi wa Mlima Kenya wakaungana dhidi yake. Rais Ruto akamteua Kindiki. Si sahihi kisiasa kudhani angekataa,” alisema Bw Kiunjuri.

Mbunge wa Manyatta Gitonga Mukunji, alisema Profesa Kindiki anajikuta upande usiopendelewa na hisia za kisiasa katika eneo hilo.

“Haiwezi kuepukika kuwa anahudumu katika serikali inayokabiliwa na upinzani mkali katika Mlima Kenya. Kwa haki au bila, anabeba lawama za serikali,” alisema.

Kwa upande wake, Mbunge wa Mbeere Kaskazini Leo Wamuthende, alisema upinzani unalenga kudhoofisha viongozi wa serikali kisiasa.

Naye Mbunge wa Gatundu Kaskazini Elijah Kururia, alisema uamuzi wa mahakama umeimarisha nafasi ya Profesa Kindiki kikatiba, akihimiza wakazi wa Mlima Kenya kumchukulia kama uwekezaji wa kisiasa wa siku zijazo.

Hata hivyo, Mwakilishi wa Kike wa Kirinyaga Njeri Maina, alisema serikali ya Rais Ruto bado inakabiliwa na upinzani mkali katika eneo hilo, jambo linalomtwika Prof Kindiki mzigo mkubwa wa kisiasa.

Utafiti wa hivi majuzi wa TIFA ulionyesha kuwa serikali ya Rais Ruto inaungwa mkono na asilimia 11 pekee katika Mlima Kenya, huku asilimia 89 wakionyesha kutoridhika nayo.

Utafiti huo huo ulipata Bw Gachagua ni kiongozi mwenye ushawishi mkubwa zaidi katika eneo hilo kwa asilimia 70.

Wachambuzi wanasema takwimu hizo zinaonyesha ukubwa wa changamoto inayomkabili Profesa Kindiki katika kujijenga kama kiongozi mkuu wa serikali katika eneo hilo kuelekea 2027.