Tiketi ya Kalonzo-Sifuna 2027 yaanza kupikwa
JUHUDI za kuunda muungano thabiti unaoweza kupambana na Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027 zinaonekana kuingia hatua mpya, kufuatia taarifa za mazungumzo kati ya kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka na kiongozi wa vuguvugu la Linda Mwananchi Edwin Sifuna.
Mahojiano kadhaa na viongozi kutoka Muungano wa Upinzani na vuguvugu la Linda Mwananchi yamefichua msukumo wa kusajili muungano utakaofahamika kama Ukombozi-Linda Mwananchi Alliance, huku Bw Musyoka na Bw Sifuna wakitarajiwa kuwa vinara wake.
Hata hivyo, huku mazungumzo yakijikita katika uwezekano wa tiketi ya Kalonzo-Sifuna, kuna jambo lingine gumu kupuuzwa: mchango wa rais mstaafu Uhuru Kenyatta.
Vyanzo vya ndani kwenye mrengo wa upinzani vinaashiria kuwepo kwa shinikizo kutoka kwa baadhi ya makundi yakipendelea ushirikiano wa Kalonzo na Fred Matiang’i, ambapo mmoja atakuwa mgombea urais na mwingine mgombea mwenza.
Pendekezo hilo linaonekana kuvutia kutokana na uwezo wake wa kupata uungwaji mkono mpana na kunufaika na mitandao inayohusishwa na rais huyo mstaafu.
Wachambuzi wa siasa wanakiri kuwa ufadhili wa kampeni utakuwa mchango mkubwa katika kubaini muungano utakaowakilisha upinzani.
Kadiri mazungumzo ya muungano yanavyoendelea, viongozi wanapima si tu umaarufu na ushawishi wa kikanda, bali pia uhalisia wa kuendesha kampeni kitaifa.
Katika mazungumzo kati ya Bw Musyoka na Bw Sifuna kuna madai kwamba yanaweza kuzaa chama kipya cha kisiasa kinachoitwa kwa muda Ukombozi-Linda Mwananchi Alliance, kilicholenga kuwaleta pamoja viongozi muhimu wa Muungano wa Upinzani na wale wa Linda Mwananchi chini ya muungano mkubwa dhidi ya Rais Ruto.
Ingawa hakuna kiongozi aliyethibitisha hadharani kuwepo kwa muungano huo, taarifa hizo zimechochea mjadala kuhusu umoja wa upinzani na juhudi za kuunda muungano thabiti wa uchaguzi wa 2027.
Taarifa hizi zinajiri huku viongozi wa upinzani wakizidisha juhudi za kuunganisha nguvu zao wakikabiliana na tamaa za kugombea urais na hesabu tata za kisiasa.
Akizungumza kabla ya ziara ya siku tatu ya upinzani eneo la Magharibi mwa Kenya inayoanza leo, kiongozi wa DAP-Kenya Eugene Wamalwa alikiri kuwa mazungumzo na viongozi wa Linda Mwananchi yanaendelea, ingawa hakuthibitisha makubaliano rasmi ya muungano.
Alisema lengo la sasa ni kuzungumza na wafuasi wao kitaifa na kujenga mwafaka kabla ya kuteua mgombea urais.
Kauli yake imechochea tetesi kuwa juhudi za kuunda muungano mkubwa dhidi ya Ruto zinaendelea kwa kasi.
Hata hivyo, baadhi ya viongozi walitoa maoni tofauti.
Seneta wa Kitui Enoch Wambua alisema hakuna sababu ya kupatia uzito mada hiyo, akisisitiza kuwa Linda Mwananchi tayari inajumuisha wanachama kutoka vyama vilivyo katika Muungano wa Upinzani.
Kwa upande mwingine, msemaji wa upinzani Mukhisa Kituyi alikanusha vikali taarifa hizo, huku Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino akisema hana ufahamu wowote kuhusu mazungumzo hayo.
Naibu mwenyekiti wa Wiper, Mutula Kilonzo Jnr naye alikanusha kuwepo kwa makubaliano rasmi, ingawa alikubali kuwa mazungumzo yanaendelea.
Huku mjadala wa muungano ukiendelea, upinzani sasa umeelekeza nguvu zake Magharibi mwa Kenya, eneo linaloonekana kuwa muhimu katika uchaguzi wa 2027.
Wamalwa alisema baada ya mvutano kati ya Rais Ruto na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, muungano wa Kenya Kwanza ulipoteza mshirika mkuu katika eneo la Mlima Kenya.
Viongozi wa upinzani wanatarajiwa kuzuru kaunti za Vihiga, Kakamega, Busia, Bungoma na Trans Nzoia katika juhudi za kuimarisha ushawishi wao.
Wanalenga pia kujiandaa kwa mkutano mkubwa utakaojadili muundo wa muungano, uteuzi wa mgombeaji na ugavi wa madaraka.
Wataalamu wanasema muungano mkubwa ni muhimu ili kushinda rais aliye mamlakani.
Wengine wanaotajwa kuwania urais ni pamoja na Kalonzo Musyoka, Fred Matiang’i, Rigathi Gachagua, Martha Karua, Justin Muturi na Eugene Wamalwa.
Hata hivyo, wachambuzi wanaonya kuwa wagombea wengi wanaweza kugawanya kura za upinzani.
Bw Sifuna ameibuka kama sura muhimu, akiungwa mkono na vijana na wanamageuzi.
Mtaalamu wa siasa Profesa Gitile Naituli anaamini kuwa Sifuna anaweza kuwa mhimili mkubwa katika siasa za 2027, akisema tiketi ya Kalonzo-Sifuna inaweza kuwa tishio kwa Rais Ruto.
Kauli hiyo inaonyesha kuwa Sifuna anaweza kuwa daraja kati ya wapigakura wa jadi wa upinzani na vijana wanaotaka uongozi mpya.
Hata viongozi wanaokataa uwepo wa muungano wanakiri ushawishi wake unakua.
Gavana wa Siaya James Orengo amewahi kusema hata Sifuna “anafaa kuwa Rais wa Kenya,” kauli iliyoongeza joto katika mjadala wa kisiasa na kuzua swali iwapo Linda Mwananchi itatoa mgombea wake wa urais.